Friday, June 5, 2009

SEHEMU YA PILI: URITHI KUTOKA KWA MUNGU

Utangulizi
Katika sehemu ya kwanza ya makala haya, tuliangalia pamoja na mambo mengine, tafsiri ya urithi, vitu ambavyo mwanadamu mmoja anaweza kuvirithi kutoka kwa mwanadamu mwenzake, watu wanaostahili, muda au wakati wa kurithi, na kadhalika.

Tunapoingia katika sehemu ya pili, ambayo inayohusu urithi kutoka kwa Mungu, lipo swali moja muhimu sana, ambalo inabidi tupate jibu lake mapema kabisa. Swali lenyewe ni je, hivi ni kweli kwamba Mungu huwa anarithisha wanadamu?

Jibu la swali hili ni muhimu kwani litatoa mwelekeo wa kile ninacholenga kuzungumzia. Tayari tumeshaona kuwa wanadamu hurithishana vitu kama mali, sura, tabia, madeni, majukumu na kadhalika. Sasa kwa upande wa Mungu mambo yanakuwaje?

Mungu hurithisha
Ninatambua kuwa wasomaji wengi wa gazeti ilio ni wakristo. Kwa sababu hiyo basi, nitatumia maandiko kadhaa ya Biblia katika kuonyesha kwamba, hata Mungu muumba wa mbingu na nchi, huwa anarithisha wanadamu mambo mbalimbali. Kwahiyo msomaji wangu naomba tufuatane kwa makini.

Tuanze kwa kusoma andiko la Agano la Kale. Katika Mithali 8:20-21 Mungu wetu anatamka kuwa, “Natembea katika njia ya haki, katikati ya mapito ya hukumu. Niwarithishe mali wale wanipendao, tena nipate kuzijaza hazina zao”.

Hapa tunaona kuwa Mungu ni wa haki, na moja ya malengo yake ni kuwarithisha mali wale wanaompenda. Kwahiyo tunaanza kupata picha kuwa Mungu huwarithisha wanadamu mali au vitu vya kushikika.

Je, Agano Jipya lina ahadi ya urithi?
Sasa hebu tutafute andiko lingine katika Agano Jipya, linaloonyesha kuwa Mungu hurithisha. Inabidi tufanye hivyo kwa sababu, ukweli ni kuwa yapo mambo ambayo yametajwa katika Agano la Kale, lakini mambo hayo hayapo au yamebadilishwa katika Agano Jipya. Mfano mzuri ni swala la kutoa sadaka za kuteketezwa au kafara za mbuzi, kondoo, ng’ombe na kadhalika.

Mambo haya yaliagizwa na Mungu katika Torati ya Musa. Lakini katika kipindi hiki cha Agano Jipya, huwa wakristo hatutoi sadaka za kuteketezwa kama ilivyokuwa zamani. Yesu alitolewa kama sadaka ya ondoleo la dhambi wakati aliposulubishwa pale msalabani (Mathayo 26:27-28).

Kwahiyo ni vema mtu anaponukuu andiko la Agano la kale, vile vile atafute andiko lingine katika Agano Jipya, ambalo linalokubaliana na kile anachokizungumzia. Vinginevyo mtu anaweza kuleta utata au upotoshaji, wakati wa kufafanua maandiko ya Biblia.

Waliookoka ni warithi wa Mungu

Tunaporudi katika mada yetu tunaweza kuona imeandikwa katika Warumi 8:16-17 kwamba, “Roho mwenyewe hushuhudia pamoja na roho zetu, ya kuwa sisi tu watoto wa Mungu; na kama tu watoto, basi tu warithi; warithi wa Mungu, warithio pamoja na Kristo.”

Wanaozungumzia katika andiko hili ni watu waliookoka; kwamba wao ni warithi wa Mungu. Loo! Ama kweli hili ni jambo zuri mno. Kumbe mtu akiokoka anapata heshima ya kuweza kurithi kutoka kwa Mungu! Saaafi kweli kweli.

Tunarithi kupitia kwa Yesu
Tunapozidi kuchunguza andiko hili tunaweza kuona kuwa watu wa Mungu wanarithi pamoja na Kristo. Swali la kujiuliza hapa ni je, hivi Bwana Yesu alirithi kitu gani kutoka kwa Mungu?

Ili kupata jibu sahihi la swali hili, nakusihi msomaji wangu usome kwa makini waraka kwa Waefeso 1:2-22. Hapa utapata picha kamili ya kile ambacho Kristo Yesu alirithi, na vile vile kile ambacho sisi wakristo tuliookoka tunaweza kurithi kupitia kwake.

Katika mistari hii tunaweza kuona kuwa Paulo anaomba waamini wafunguke macho yao ya rohoni, ili watambue uzuri wa kuokoka “na utajiri wa utukufu wa urithi wake (yaani Mungu) katika watakatifu jinsi ulivyo (mstari wa 18).

Katika mstari wa 20-22 tuunaweza kuona jinsi Mungu alivyomtukuza Kristo baada ya kumfufua katika wafu, halafu akavitia vitu vyote chini ya miguu yake, akamweka awe kichwa juu ya vitu vyote kwa ajili ya kanisa”. Yaani kila kitu alichokabidhiwa Bwana Yesu ni kwa ajili ya kanisa lake au wale waliomwamini kwa njia ya kuokoka.

Ni vitu gani tunavyoweza kurithi kutoka kwa Mungu?

Sasa baada ya kupata uthibitisho kuwa Mungu huwa anarithisha, hebu sasa tujiulize swali jingine. Je, ni vitu gani ambavyo sisi wanadamu tunaweza kuvirithi kutoka kwa Mungu wetu? Je, vitu hivyo vinafanana na vile ambavyo tunarithi kutoka kwa wanadamu au wazazi wetu?

Ukweli ni kuwa yapo mambo tunayorithishana sisi wanadamu, ambayo kwa namna fulani yanafanana na yale tunayoweza kurithi kutoka kwa Mungu. Lakini mengine ni tofauti kabisa, na wala hayawezi kupatikana kwa wanadamu. Nitafafanua jambo hili kadri tunavyosonga mbele na makala haya.

Tunarithi kufanana na Mungu.
Katika sehemu ya kwanza ya makala haya, nilieleza kuwa moja ya mambo ambayo mtu anaweza kurithi kutoka kwa mwenzake ni vitu kama sura, au tabia, au maumbile na kadhalika. Nilionyesha jinsi ambavyo baada ya anguko, Adamu alimzaa mwana aliyefanana naye (Mwanzo 5:3).

Moja ya mambo ambayo mwanadamu anaweza kuyarithi kutoka kwa Mungu ni kule kufanana na huyu Muumba wake. Katika Warumi 8:29 imeandikwa kuwa, “Maana wale aliowajua tangu asili, aliwachagua tangu asili wafananishwe na mfano wa Mwana wake, ili yeye (Bwana Yesu) awe mzaliwa wa kwanza miongoni mwa ndugu wengi”.

Wanaozungumziwa hapa ni watu waliookoka; kwamba baada ya kuokoka, wanabadilishwa na kuanza kufanana na Yesu. Sote tunafahamu kwamba Kristo ni mfano wa Mungu (Wakolosai 1:15). Ni chapa ya Mungu (Waebrania 1.3).

Yesu Kristo mwenyewe alisema kwamba yeye na Mungu ni kitu kimoja, na kwamba Mungu yu ndani yake na yeye ndani ya Mungu (Yohana 14:8-13, Yohana 17:20-23). Kwahiyo kufanana na Yesu ni sawa na kufanana na Mungu. Hiki ndicho kinachotokea mtu anapookoka..

Tunarithi tabia za Kiungu au nia ya Mungu
Msomaji utakumbuka kuwa katika sehemu ya kwanza ya makala haya nilisema kuwa moja ya vitu ambavyo mtu anaweza kurithi kutoka kwa wazazi wake ni tabia nzuri kama vile upole, ukarimu, huruma; au tabia mbaya kama uchoyo, usengenyaji, hasira, ugomvi na kadhalika.

Ni ajabu kuwa sisi wanadamu tunaweza kurithi tabia za Kiungu. Bahati nzuri tabia hizi ni njema tu siku zote. Hazikuchanganyika nzuri na mbaya, kama inavyotokea pale tunaporithi tabia za wazazi wetu .

Mwanadamu anapookoka, Roho wa Mungu huanza kukaa ndani yake. Huyo Roho ndiye anayemwezesha kuwa na tabia za Kiungu. Katika Wagalatia 5:22-23 tunaambiwa kuwa, “Lakini tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi”

Hili tunda la Roho linalozungumziwa hapa ni matokeo ya kumkubali Yesu Kristo kuwa Bwana na Mwokozi wa maisha yako. Ni mambo ambayo mtu huyapokea kutoka kwa Roho Mtakatifu. Huu ni urithi kutoka kwa Mungu, kwani Roho Mtakatifu ni Mungu mwenyewe.

2 maoni:

Anonymous said...

kama marehemu aliacha wosia na aliechaguliwa kusimamia wosia anapendelea upande mm0ja na ataki kufungua mirathi mpaka sasa tokea mwaka jana mwezi8... kisheria tutafanyaje!!

Anonymous said...

na kama marehemu alikuwa na kesi mahakamani na hizo je mirathi ikifunguliwa si itawekewa kipingamizi!!

Post a Comment

Tafadhali kuwa mstaarabu.
Jiheshimu kwa kutokuacha maneno yenye kauli ya kutusi ama kuudhi wengine.
Maoni yasiyofaa hayatachapishwa.

TaCHe & Subi.nukta77 chose to wear BlueWeed by BlogOh!Blog | to Blogger by Gre at Template-Godown | Entries (RSS) and Comments (RSS).