Friday, June 5, 2009

URITHI: Hitimisho



Kwa sasa nimefikia mwisho kabisa wa mada hii inayohusu urithi. Naomba nihitimishe kwa kusisitiza mambo yafuatayo.

Kwetu sisi wanadamu, Mungu ni kama walivyo baba zetu hapa duniani. Kama ambavyo wazazi wetu waliotuzaa huturithisha mali, vile vile Mungu naye huwarithisha wanadamu baraka za aina mabalimbali.

Wapo watu maalumu wataostahili kurithi. Sio kwamba kila mtu anaweza kupewa urithi. La hasha. Wana ndio warithi halali wa mali za wazazi wao.

Mungu naye ana wana. Watu waliozaliwa mara ya pili, au waliookoka, hao ndio wana wa Mungu. Hao ndio wanaostahili kurithi baraka kutoka kwake.

Urithi kutoka kwa mwanadamu mmoja kwenda kwa mwanadamu mwingine una sheria, kanuni au taratibu zinazosimamia jambo hili. Hali kadhalika, urithi au baraka kutoka kwa Mungu una kanuni au masharti au taratibu zake.

Ili mtu aweze kurithi mali au baraka, ni lazima atimize masharti yanayotakiwa. Ni lazima atimize wajibu wake. Hakuna haki isiyokuwa na wajibu.

Mali yote wanayochuma wazazi huwaachia au huwarithisha wana wao. Kadhalika, kila alichoumba Mungu, ni kwa ajili ya mwanadamu, hasa wale wanaolicha jina lake. Yaani wale waliookoka.

Kama ambavyo mzazi huona fahari kumrithisha mwanawe mali, vile vile Mungu hufurahi sana wana wake wanapofanikiwa au wanapobarikiwa. Kiu ya Mungu ni kuona wanadamu wote wanaishi maisha ya fanaka. Ndio maana huwarithisha mali (Mithali 8:17-21).

Watu wengi, au tuseme wana wa Mungu, wanashindwa kurithi baraka kutoka kwake kwa sababu ya kutotimiza masharti yanayoambatana na baraka hizo.Wapo wengine wanaozitaka, lakini hawamtaki mwenye kuzimiliki. Hawataki kufanyika wana wa Mungu au kuokoka.

Kundi kubwa la waumini wanaoshindwa kurithi baraka kutoka kwa Mungu ni wale wasiofuata kanuni au wasiotekeleza masharti yanayoambatana na baraka wanazozitaka. Wengi hawamtolei Mungu kiasi cha kutosha au hawamtumikii kabisa, lakini bado wanataka kubarikiwa.

Msomaji ni matumaini yangu kuwa mada hii imekufungua macho kiasi cha kutosha. Kama ni urithi kutoka kwa wanadamu, naaamini sasa unatambua haki zako, na vile vile wajibu wako. Kwahiyo unajua la kufanya ili usipoteze haki hiyo.

Kama ni baraka kutoka kwa Mungu, napo naamini kwa sasa unatambua mambo unayoweza kupokea kutoka kwake, na vile vile wajibu wako au mambo unayotakiwa kuyafanya ili ubarikiwe kwa vitu vya rohoni na vya mwilini.

Rai yangu ni hii. Kama kuna eneo ambalo umegundua kuwa ulikuwa na mapungufu, tafadhali lifanyie kazi. Lirekebishe.

Kumbuka kuwa kama baba yetu wa duniani anavyompenda mwanawe, Mungu wetu naye ni mwema sana na siku zote anatuwazia yaliyo mema sisi tulio wana wake. Ukiona hayo mema aliyoahidi hayakufikii, ujue tatizo sio Yeye, bali ni wewe. Jirekebishe.

Lishike sana neno hili, :”Mungu si mtu, aseme uongo; wala si mwanadamu ajute; Iwapo amesema hatalitenda? Iwapo amenena, hatalifikiliza? (Hesabu 23:19). Wewe timiza wajibu wako, halafu usubiri wakati wa Bwana. Uwe mvumilivu, nawe utarithi baraka. Asante sana na Mungu wa mbinguni akubariki. Amen. Read More......

URITHI: Ulimwengu uliumbwa kwa ajili ya mwanadamu


Mungu anapoturithisha baraka mbalimbali ni kwamba, anakuwa anaturudishia kile kilichokuwa stahili yetu tangu kuumbwa kwa ulimwengu huu. Ni kweli Biblia inasema kuwa Shetani ni mungu au mtawala wa dunia hii (2Wakorintho 4:4, Luka 4:6).

Shetani aliipata haki ya kuitawala dunia baada ya anguko la Adamu na Hawa, pale waliposhindwa kutii agizo la Mungu, wakala matunda ya mti waliokuwa wamekatazwa (Mwanzo 3:1-19). Lakini tangu mwanzo, mwanadamu ndiye aliyetawazwa juu ya uumbaji wa Mungu (Zaburi 8:3-8).

Mwanadamu ndiye mlengwa wa uumbaji wa Mungu
Ukweli ni kuwa mwanadamu ndiye mlengwa (focal point) wa kila alichoumba Mungu. Yeye ndiye aliyetawazwa juu ya vitu vyote (Mwanzo 1:26, Zaburi 8:4-8), ili avimiliki na kuvitumia kwa manufaa yake. Haya mahangaiko au uhitaji tulio nao hapa dunia haukuwa mpango wa Mungu hata kidogo.

Ni kweli kulitokea anguko la mwanadamu, akapoteza mamlaka aliyopewa na Mungu juuya ulimwengu huu.. Lakini baada ya Yesu kuja duniani, na hatimaye kufa pale msalabani, Mungu aliweka vitu vyote mikononi mwake (Waebrania 1:2-4). Biblia inatuambia kuwa Mungu, “akavitia vitu vyote chini ya miguu yake, akamweka awe kichwa juu ya vitu vyote kwa ajili ya kanisa” (Waefeso 1:22).

Kifo cha Yesu pale msalabani kilirejeza kwa kiwango fulani mamlaka ambayo mwanadamu alikuwa nayo tangu mwanzo. Kwa njia ya Yesu, watu waliookoka wanaweza kumnyang’anya Shetani kile kitu au mamlaka aliyoyapata kwa ujanja (Mwanzo 3:1-7).

Sio mapenzi ya Mungu wanadamu waishi kwa taabu
Sababu ya pili inayomfanya Mungu aturithishe baraka ni ili tuishi kwa furaha na amani.. Ni kutokana na upendo alio nao kwetu sisi wanadamu. Katika Yohana 16:24 Yesu anatuambia kuwa, “Hata sasa hamkuomba neno kwa jina langu; ombeni, nanyi mtapata; furaha yenu iwe timilifu”. Unaweza kuona hapa kuwa Yesu anasema kuwa tukiomba tutapata ili tufurahi.

Ukweli ni kuwa sio mapenzi ya Mungu sisi wanadamu tuishi kwa taabu. Sio mpango wake tuugue, au tulale njaa, au tupungukiwe chochote, na kadhalika. La hasha. Hayo ni matokeo ya anguko la mwanadamu, au tuseme ni matokeo ya dhambi.

Mungu hufurahia mafanikio ya watu wake
Katika Zaburi 35:27 tunaambiwa kuwa, “Washangilie na kufurahi, wapendezwao na haki yangu. Naam, waseme daima, Atukuzwe BWANA, apendezwaye na amani ya mtumishi wake”. Maneno haya katika Biblia ya Kiingereza yanasomeka hivi, “Let them shout for joy and be glad, who favour my righteous cause; and let them say continually, ‘Let the Lord be magnified, who has pleasure in the prosperity of his servant”.

Maneno ‘who has pleasure in the prosperity of his servant’ yana maana kuwa, Mungu hufurahi sisi wanadamu tunapofanikiwa au tunapobarikiwa. Na kama nilivyosema, hii ni moja ya sababu inayomfanya aturithishe baraka za namna mbalimbali.

Ni kwa jinsi gani tunaweza kurithi baraka kutoka kwa Mungu?
Nafikiri makala haya haya hatakamilika bila kueleza, ni kwa jinsi gani sisi wanadamu tunavyoweza kurithi baraka kutoka kwa Mungu. Msomaji utakumbuka kuwa huko nyuma niliainisha baadhi ya sababu au vikwazo vinavyoweza kuwazuia watu wa Mungu wasirithi baraka kutoka kwake.

Kwa kukumbushia nilisema kuwa vikwazo hivyo ni kama ifuatavyo;
  1. Mwamini kuendelea au kubaki kuwa mtoto mchanga.
  2. Kutokujua haki zetu au mambo tunayostahili kurithi.
  3. Kutotambua na kutekeleza masharti yaliyoambatana na kila aina ya baraka.
  4. Kutotembea au kutotumikia wito
Baada ya kuokoka, unatakiwa ukue
Nafikiri sasa tunaweza kukubaliana kuwa, ili mtu aweze kurithi baraka ni lazima aondoe vikwazo vilivyo mbele yake. Ni lazima atimize masharti yanayotakiwa. Kitu cha kwanza ni lazima afanyike mwana. Ni lazima azaliwe mara ya pili. Yaani ni lazima aokoke.

Kama tulivyoona huko nyuma, Mungu ni kama alivyo baba yetu wa hapa duniani. Kwa kawaida, baba huwa hamrithishi mali kila mtoto anayemwona. Hapana. Huwarithisha wanawe tu aliowazaa.

Vivyo hivyo Mungu naye huwarithisha wanawe. Na kama tulivyoona, wana wa Mungu ni wale waliookoka. Hao ndio wanaoweza kurithi baraka kutoka kwake.

Baada ya kufanyika mwana, ni lazima mwamini akue. Hatakiwi kuendelea kuwa mtoto mchanga kiroho. Ni lazima amjue sana Mungu (Ayubu 22:21), ajue neno lake kwa wingi (Wakolosai 3:16), awe imara katika imani (2Petro 1:10) na kadhalika. Sio mtu anasema ameokoka, lakini ni mbumbumbu katika katika maswala yanayohusu ufalme wa Mungu.

Ukikua utatambua haki na wajibu wako
Mwamini akikua, ndipo anaweza kutambua haki zake. Ndipo anaweza kutambua mambo ambayo anastahili kupokea au kurithi kutoka kwa Mungu. Akiisha kuyatambua, ndipo anaweza kuyadai au kuyaomba.

Biblia inatuambia kuwa tusisumbuke, “Bali utafuteni kwanza ufalme wake (yaani wa Mungu), na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa” (Mathayo 6:33). Kuutafuta ufalme wa Mungu ni kukubali kuokoka na vile kujifunza kwanza yale mambo yanayohusu ufalme huu. Baada ya hapo ndio unaweza kubarikiwa.

Mwamini anapokua, ndipo anaweza kutambua kanuni za kubarikiwa. Ndipo atatambua masharti yaliyoambatana na kila aina ya baraka. Ndipo atatambua wajibu wake au mambo anayotakiwa ayakamilishe, kabla hajabarikiwa. Vinginevyo atabaki anashangaa tu ni kwanini haoni baraka za Mungu katika maisha yake?

Tambua wito wako
Tumeona kuwa baraka nyingi za mwamini zimefungamanishwa ndani ya wito wake. Kwahiyo ni muhimu kila mtu aliyeokoka atambue wito au ile kazi maalumu ambayo Mungu anamtarajia aifanye hapa duniani. Na kusema kweli jambo hili sio rahisi hata kidogo.

Kazi ya kutambua wito sio nyepesi. Inahitaji mafunzo maalumu. Vile vile mwamini anatakiwa autafute uso wa Bwana kwa bidii, hadi hapo atakapopata jibu la uhakika kwamba anatakiwa afanye nini (Zaburi 32;8, Zaburi 143:8). Yawezekana jambo hili likachukua hata miaka zaidi ya kumi kabla jibu halijapatikana.

Uwe mvumilivu
Mwisho kabisa, pamoja na kutekeleza masharti yote yanayotakiwa, ni lazima mwamini awe mvumilivu. Ukweli ni kuwa baraka za Mungu huwa haziji kirahisi au kiulaini, kama watu wengi wanavyodhani. Kuna kuvumulia. Na hapa ndipo wengi wetu tunapokwama.

Siku hizi waumini wengi hawana uvumilivu. Hawataki kusubiri. Wanataka baraka za chapu chapu tu. Wakitoa sadaka leo, au wakimtumikia Mungu kidogo tu, au wakiombewa leo, wanataka kesho yake waone baraka. Mambo hayako hivyo ndugu zanguni.


Ibrahimu alivumilia
Ili jambo hili lieleweke vema, hebu tuangalie mifano michache ya watu waliovumilia kwa muda mrefu hadi wakabarikiwa au wakapokea ahadi walizoahidiwa na Mungu. Tuanze na Ibrahimu, baba yetu wa imani.

Wasomaji wazuri wa Biblia wanafahamu kuwa Mungu alianza kuongea na Ibrahimu wakati alipokuwa na umri wa miaka sabini na tano (Mwanzo 12:4). Lakini ilipita miaka ishirini na mitano, ndipo ahadi ya kupata mtoto ilipotimia, yaani wakati Ibrahimu akiwa mzee wa miaka mia moja (Mwanzo 17:17).

Sasa ndugu yangu, kusubiri ahadi ya BWANA kwa muda wa miaka ishirini na mitano sio jambo dogo. Yahitaji moyo mkuu. Yahitaji uvumilivu wa hali ya juu. Huo ndio ukweli wenyewe.

Kwa bahati nzuri baba yetu wa imani alishinda mtihani huu wa uvumilivu. Biblia inatuambia kuwa, “Kwa maana Mungu, alipompa Ibrahimu ahadi, kwa sababu alikuwa hana mkubwa kuliko yeye mwenyewe wa kumwapa, aliapa kwa nafsi yake. Akisema, Hakika yangu kubariki nitakubariki. Na hivyo kwa kuvumilia akaipata ile ahadi (Waebrania 6:13-15).

Yusufu alivumilia
Mfano mwingine wa uvumilivu ni wa Yusufu. Nafikiri wengi wetu tunafahamu historia ya ndugu huyu, jinsi alivyoota ndoto kwamba ipo siku baba yake, mama yake na ndugu zake watakuja kumsujudia (Mwanzo 37:5-11). Jambo hili halikutimia haraka, wala kirahisi.

Biblia inatuonyesha kuwa Yusufu alikuwa na umri wa miaka kumi na saba wakati alipoota ndoto zile (Mwanzo 37:2). Ilimchukua miaka kumi na mitatu hadi alipokuwa Waziri Mkuu wa Misri, wakati huo akiwa na umri wa miaka thelathini (Mwanzo 41:46).

Baada ya kuwa Waziri Mkuu, ilipita miaka mingine zaidi ya saba, ndipo ahadi ya BWANA ilipotimia. Ndipo baba yake na ndugu zake walipokuja kukaa chini ya himaya yake, wakati walipohamia Misri njaa ilipopamba moto katika nchi ya Kanaani (Mwanzo 46:1-26).

Daudi alivumilia
Mfano wa mwisho ni wa mfalme Daudi. Msomaji ukifuatilia maisha ya Daudi utagundua kuwa alipakwa mafuta (ili awe mtawala badala ya Sauli) wakati akingali kijana mdogo tu, mchunga kondoo (1Samweli 16:1-13).

Ilipita miaka mingi sana kabla hajawa mfalme wa Israeli. Biblia inatuambia kuwa, “Daudi alikuwa amepata miaka thelethini alipoanza kutawala, akatawala miaka arobaini” (2 Samweli 5:4). Hapa katikati Daudi alivumilia misukosuko au mapito mengi kabla hajapata fursa ya kutawala.

Usichoke; usikate tamaa
Ninachotaka kusema ni hiki msomaji wangu. Ijapokuwa Mungu amekuahidi jambo fulani, inaweza kupita miaka mingi sana kabla jambo hilo halijatimia. Unaweza kuahidiwa baraka kama ilivyokuwa kwa Ibrahimu, lakini vile vile unaweza kupita muda mrefu sana kabla baraka hizo hazijatimia katika maisha yako.

Ndio kusema mwamini anatakiwa awe na uvumilivu. Hiki ndicho Kinachozungumzwa katika Waebrania 6:11-12 kwamba, “Nasi twataka sana kila mmoja wenu aidhihirishe bidii ile ile, kwa utimilifu wa matumaini hata mwisho; ili msiwe wavivu, bali mkawe wafuasi wa hao wazirithio ahadi kwa imani na uvumilivu”

Huko nyuma nilisema kuwa mwamini hawezi kuwa na uhakika ni lini atakapobarikwa na Mungu, hata baada ya yeye kutimiza masharti yote yanayotakiwa. Anatakiwa asubiri wakati wa Bwana. Hicho ndicho tunachoambiwa katika Wagalatia 6:9 kwamba, “Tena tusichoke katika kutenda mema; maana tutavuna kwa wakati wake, tusipozimia roho”.

Hizi baraka za papo kwa papo zinazohubiriwa na mitume au manabii wengi wa siku za leo sio mpango kamili wa Mungu. Nyingi ni kiini macho. Ni usanii. Mwenye sikio la kusikia na asikie. Read More......

TaCHe & Subi.nukta77 chose to wear BlueWeed by BlogOh!Blog | to Blogger by Gre at Template-Godown | Entries (RSS) and Comments (RSS).