Friday, June 5, 2009

Watu wa Mungu waliofanikiwa ni wachache

Ninakubali kunaweza kuwepo walokole wachache waliofanikiwa kimaisha, lakini si chochote wala si lolote, ukilinganisha na utajiri au mafanikio ya watu ambao hawajaokoka. Nataka tujiulize tena; kwanini hali iko hivi?

Naomba sote tutafakari. Kwanini watu wa Mungu wanaonekana kama vile hawana kitu wakati dunia na vyote viijazavyo ni mali ya Baba yao wa mbinguni? (Zaburi 24:1). Biblia inatuambia kuwa Mungu aliweka vitu vyote chini ya miguu ya mwanawe Yesu kwa ajili ya kanisa au watu waliookoka (Waefeso 1:22).

Sasa kama sisi tuliookoka tumeahidiwa baraka nyingi namna hiyo, inakuwaje hatuonekani kama watu waliobarikiwa? Tatizo liko wapi? Je, Mungu ni mwongo anapoahidi kuturithisha baraka au kuna mahali ambapo sisi watu wake tumekosea?

Katika makala haya nitajaribu kueleza sababu takribani nne, ambazo binafsi ninaamini ndizo zinazowafanya waumini wengi washindwe kurithi baraka kutoka kwa Mungu wao. Kwahiyo msomaji naomba tufuatane kwa makini katika eneo hili.

Kutokujua haki zetu
Moja ya mambo ambayo yanawafanya watu wa Mungu wasiweze kurithi baraka ni kutotambua haki zao. Ni ujinga wa kutotambua ni vitu gani na kwa kiwango gani wanaweza kurithi au kupokea kutoka kwa Mungu. Na kwa sababu hiyo wanashindwa kuomba au kudai haki hizo.

Katika Isaya 43:26 Mungu anatuambia sisi watu wake hivi, “Unikumbushe, na tuhojiane; eleza mambo yako, upate kupewa haki yako”. Hapa tunahimizwa tudai haki zetu kutoka kwa Mungu. Sasa utawezaje kudai haki ambayo huifahamu? Haiwezekani kabisa. Na hili ndio tatizo linalowakumba baadhi ya watu waliookoka. Hawajui haki yao ya kubarikiwa.

Katika sehemu ya kwanza ya makala haya, iliyohusu urithi kutoka kwa mwanadamu mmoja kwenda kwa mawanadamu mwingine, nilisema kuwa moja ya mambo yanayowafanya warithi halali wa marehemu wasipate mali iliyoachwa ni kutotambua haki yao na taratibu za kupata haki hiyo.

Ni ajabu kuwa hata tunapoangalia urithi kutoka kwa Mungu, hali ni hiyo hiyo. Wapo waumni wasiojua haki zao za kurithi baraka na mambo ya kufanya au wajibu wao, ili waweze kupewa haki hizo. Na kwa sababu hiyo wanaendelea kuwa maskini wa vitu vya rohoni na vya mwilini.

Tambua haki zako
Hebu tuanze kwa kuangalia baraka za rohoni. Tayari tumeshaona kuwa ujazo wa Roho Mtakatifu ni ahadi au haki ya kila mtu aliyeokoka. Cha ajabu makanisani mwetu wapo wakristo waliookoka, lakini bado hawajapokea ahadi ya kujazwa Roho Mtakatifu.

Tatizo la wakristo kama hawa sio kwamba hawataki kujazwa. La hasha. Wapo wanaodhani kuwa jambo hili halipo kabisa kwa kanisa la leo. Wanadhani hayo ni mambo yaliyolihusu kanisa la mwanzo tu, lile kanisa la enzi za Matendo ya Mitume.

Wapo wakristo wanaodhani kuwa ujazo wa Roho Mtakatifu upo, ila ni kwa ajili ya watu maalumu tu. Wao wanafikiri kwamba hawahusiki kabisa na jambo hili. Maskini watu hawa, yaani wamekosea kweli. Kujazwa ni haki ya kila mwamini (Mdo 2:17-18). Huo ndio ukweli.

Kwa sababu ya kutatambua haki ya kila mwamini kujazwa nguvu za Roho Mtakatifu, yapo makanisa yasiyozungumzia au kufundisha jambo hili katikati ya makusanyiko yao. Unaweza kukutana na waumini wanaodai kuwa wameokoka, lakini ukizungumzia habari ya ujazo wa Roho Mtakatifu au kunena kwa lugha, hawakuelewi kabisa.

Tatizo la ujinga ni la miaka mingi
Hebu tugeukie Biblia tuone jinsi tatizo hili lilivyojitokeza katika kanisa la mwanzo. Tunasoma katika Matendo ya Mitume 19-1-2 kuwa, “Ikawa, Apollo alipokuwa Korintho, Paulo, akiisha kupita kati ya nchi za juu, akafika Efeso; akakutana na wanafunzi kadha wa kadha huko; akawauliza, Je! Mlipokea Roho Mtakatifu mlipoamini? Wakamjibu, La, hata kusikia kwamba kuna Roho Mtakatifu hatukusikia”.

Msomaji unaweza kuona jinsi hawa waumini walivyokuwa wameokoka, lakini hawakujua kama kuna kitu kama kujazwa Roho Mtakatifu? Vile vile hawakujua ubatizo sahihi wa Kibiblia (Matendo 19:3-5). Tatizo kama hili laweza kuwepo katika makanisa ya leo. Usitegemee waumini walio chini ya kanisa au huduma ya namna hii waweze kupokea ahadi ya Roho Mtakatifu.

Kinachofurahisha katika lile kanisa alilokutana nalo Paulo ni kwamba, aliwafundisha ubatizo sahihi na habari ya ujazo wa Roho Mtakatifu. Biblia inatuambia kuwa, “Na Paulo, alipokwisha kuweka mikono yake juu yao, Roho Mtakatifu akaja juu yao; wakaanza kunena kwa lugha, na kutabiri” (Matendo 19:6).

Ni haki yako kumpokea Roho Mtakatifu
Yawezekana wewe unayesoma makala haya umeokoka, lakini hujajazwa Roho Mtakatifu. Yawezekana jambo hili halitajwi wala halifundishwi hapo mahali unaposali. Pengine utendaji wa huyu Roho wa Mungu au miujiza haionekani kabisa hapo kanisani mwako.

Sikiliza nikwambie kitu ndugu yangu. Ni haki yako kupokea ahadi au baraka ya Roho Mtakatifu. Ni haki yako kujazwa. Hili lipo wazi kabisa, “Kwa kuwa ahadi hii ni kwa ajili yenu, na kwa watoto wenu, na kwa watu wote watakaoitwa na Bwana Mungu wetu wamjie” (Matendo 2:39).

Karama na vipawa ni sehemu ya kanisa
Tunapokuja katika karama na vipawa mbalilmbali tunakuta kuwa hali ndiyo ili ile ya ujinga wa kutofahamu. Wapo waumini wasiojua kuwa mambo haya yapo na kwamba hata wao wanaweza kupokea baraka hizi. Kwamba wanaweza kuwa na karama au kipawa fulani.

Yapo makanisa au waumini wasiojua kuwa karama na vipawa ni nyenzo muhimu sana katika kuifanya kazi ya Bwana, na kwamba vitu hivi vinatakiwa vionekane katika makusanyiko ya watu wa Mungu. Kwa sababu ya kutofahamu, makanisa yao na wao binafsi wanadumaa kiroho. Hawaoni ishara na maajabu katika yao Marko 16:17, Matendo 14:3).

Usiringe na karama au kipawa ulicho nacho
Baadhi ya waumini au watumishi waliojaliwa kuwa na karama au kipawa fulani, wamevitaifisha. Kwanza kabisa wapo wanaoringa navyo. Wanajikweza. Halafu wapo wengine ambao hawawaambii wenzao jambo hili. Hawawafundishi wala hawatumii baraka hizi kwa manufaa ya waumini wenzao.

Kuhusu utendaji wa karama tunaambiwa hivi katika 1Wakorintho 12:4-11, “Basi pana tofauti ya karama, bali Roho ni yeye yule. Tena pana tofauti ya huduma, na Bwana ni yeye yule. Kisha pana tofauti za kutenda kazi, bali Mungu ni yeye yule azitendaye kazi zote katika wote. Lakini kila mmoja hupewa ufunuo wa Roho kwa kufaidiana. Maana mtu mmoja kwa Roho apewa neno la hekima; na mwingine neno la maarifa, apendavyo Roho yeye yule; mwingine imani katika Roho yeye yule; na mwingine kupambanua roho; mwingine aina za lugha; na mwingine tafsiri za lugha; lakini kazi hizi zote huzitenda Roho huyo mmoja, yeye yule, akimgawia kila mtu peke yake kama apendavyo yeye”.

Karama hutoka kwa Mungu
Msomaji nnachotaka uzingatie katika mistari hii niliyonukuu ni kuwa, chanzo cha karama ni Mungu mwenyewe. Mstari wa 7 unasema ‘lakini kila mmoja hupewa ufunuo wa Roho kwa kufaidiana’. Lengo la karama ni kushirikishana na kusaidiana. Sio kuringiana au kunyanyasana nazo, kama baadhi ya watumishi wa Mungu wanavyofanya katika siku za leo.

Mstari wa 11 unamalizia kwa kusema ‘lakini kazi hizi zote huzitenda Roho huyo mmoja, yeye yule, akimgawia kila mtu peke yake kama apendavyo yeye”. Yaani Roho Mtakatifu ndiye mmiliki na msimamizi wa matumizi ya karama, na kwamba huzigawa kama apendavyo na sio kama mwamini anavyotaka.

Hali ilivyo katika makanisa mengi duniani ni kwamba, kuna waumini au watumishi ambao wanatamani sana kama wangekuwa na karama au kipawa fulani. Wengine wakivikosa, hulazimisha mambo. Unakuta mtu anajiita mtume na nabii, au anaingia katika huduma ya uchungaji au uinjilisti, wakati hana kibali cha Roho Mtakatifu. Hili ni kosa kubwa mno.

Kutokujua wajibu au masharti au taratibu au kanuni za kubarikiwa
Tatizo la pili linalolikabili kanisa la leo, na kwa sababu hiyo wanashindwa kubarikiwa, ni kutokujua kwamba kila haki imeambatana na masharti au wajibu. Hali ilivyo sasa hivi ni kuwa, walokole wengi wanakimbilia kudai haki ya kubarikiwa kabla ya kutimiza masharti, taratibu na kanuni zilizowekwa na Mungu kabla hajatoa (release) baraka hizo.

Sasa hivi tunashuhudia wimbi la waumini ambao nitawaita wakimbizi au wahamiaji. Hawa ni watu waliookoka vizuri kabisa, lakini wanahama kutoka kanisa moja la kilokole na kuhamia kwenye kanisa lingine la kilokole.

Ni waumini wanaohama kutoka kwa mchungaji huyu, au mtume huyu, au nabii huyu, au huduma hii, na kuhamia kwenye kikundi kingine cha kilokole. Swali la kujiuliza ni kwanini tuna wakimbizi au wahamiaji wa kikristo? Ni kwanini tuna walokole wanaohamahama ovyo?

Kuna uhamaji unaokubalika
Ninatambua kuwa kuna uhamaji ambao una sababu za msingi zinazokubalika. Uhamaji huu ni pamoja na waumini wanaotoka katika makanisa yasiyohubiri au yanayopinga dhana ya kuokoka. Ni pamoja na waumini wanaohamishwa kikazi au wanaohamia kwenye makazi mapya, na kwa sababu hiyo wanalazimika kutafuta kanisa la kilokole lililo karibu na mahali walipohamia.

Sasa wakimbizi ninaotaka kuzungumzia sio waumini wanaohama kwa sababu zinazokubalika. Hapana. Ni walokole wanaohama kwa sababu ya kutodhirika na mahali walipokuwa. Unakuta wala hawajafukuzwa, wala hakuna aliyewaudhi, lakini wanahama.

Hakuna kubarikiwa kabla ya kutimiza wajibu
Sikiliza msomaji. Moja ya sababu kubwa inayowafanya walokole wahame ovyo ovyo ni kiu ya kutafuta baraka za Mungu. Wanakaa katika kanisa moja au huduma fulani kwa muda, halafu wanaona kama vile hawabarikiwi. Na hapa nina maana kuwa hawaoni baraka za mwilini.

Ukizidi kuchunguza kiini cha uhamaji ninaozungumzia utakuta kuwa, tatizo kubwa ni waumini hao kushindwa kutimiza wajibu wao au masharti yanayoambatana na baraka wanazohitaji au walizoahidiwa na Mungu kupitia neno lake..

Hali ilivyo kwa sasa ni kwamba, walokole wengi wanataka au wanadai haki ya kubarikiwa, lakini hawataki kutimiza wajibu wao. Hawataki kumtumikia Mungu; hawataki kutoa sadaka au wanatoa kidogo sana; hawafanyi kazi, na kadhalika. Hili ndio tatizo kubwa la kanisa la leo.

Nimeshasema huko nyuma, na sasa narudia tena. Hakuna baraka au ahadi ya Mungu isiyo na masharti. Yapo mambo ambayo mwamini anatakiwa ayatimize, ndipo aweze kubarikiwa. Vinginevyo atabaki kuwa mkimbizi wa baraka katika maisha yake yote ya wokovu.

Mwamini mkimbizi asipokuwa makini, Yesu atakaporudi mara ya pili anaweza kumkuta barabarani akiwa bado anahama kutoka sehemu moja ya kilokole, akielekea sehemu nyingine. Mtu kama huyu asidhani kuwa anaweza kuziona baraka za Mungu. Ni mahangaiko matupu.

Baraka zinakuja; hazifuatwi
Ngoja nimalizie kipengele hiki kwa kusema hivi. Baraka hazifuatwi; hazitafutwi makanisani au kwenye huduma. Baraka hazitoki kwa mchungaji, mtume au nabii fulani. Hapana. Baraka zitakufuata mahali popote pale utakapokuwa, ali mradi umetimiza mashari au wajibu wako unaohusiana na baraka hizo.

Ninakubali kuwa makanisani au kwenye huduma tunaweza kufundishwa na wachungaji wetu, au hao mitume na manabii, namna ya kubarikiwa. Lakini wao sio wanaozigawa. Wao wanapaswa kutuelezea baraka hizo na masharti yake. Baada ya kuyatimiza, ndipo tunaweza kubarikiwa mahali popote pale tutakapokuwa.
Utabarikiwa popote pale utakapokuwa

Msomaji nakuomba usome tena kwa makini Kumbukumbu la Torati 28:1-14, ambapo zimeorodheshwa baraka tele, pamoja na masharti yake. Mstari wa 2 unasema kuwa, “na baraka hizi zote zitakujilia na kukupata usikiapo sauti ya BWANA, Mungu wako”

Unaweza kuona kuwa baraka zitakujilia, au zitakufuta (shall come upon you). Sio wewe unakimbizana nazo kutoka kanisa hili hadi jingine, au mtume huyu hadi yule, na kadhalika. Ndio maana Biblia inasema kuwa ‘utabarikiwa mjini, utabarikiwa na mashambani’ (mstari wa 3).Vile vile ‘utabarikiwa uingiapo, utabarikiwa na utokapo” (mstari wa 6).

Kinachotakiwa kwako ni kuisikia sauti ya Mungu. Sio unahama bila hata kuwasiliana Naye, ili akuruhusu. Matokeo yake unabaki kuwa mkimbizi. Na sote nadhani tunafahamu hali za wakimbizi popote pale walipo. Kwa kweli sio nzuri. Hali zao ni mbaya. Nami nisingetaka hali yako iwe mbaya.

0 maoni:

Post a Comment

Tafadhali kuwa mstaarabu.
Jiheshimu kwa kutokuacha maneno yenye kauli ya kutusi ama kuudhi wengine.
Maoni yasiyofaa hayatachapishwa.

TaCHe & Subi.nukta77 chose to wear BlueWeed by BlogOh!Blog | to Blogger by Gre at Template-Godown | Entries (RSS) and Comments (RSS).