Friday, June 5, 2009

URITHI: Hitimisho



Kwa sasa nimefikia mwisho kabisa wa mada hii inayohusu urithi. Naomba nihitimishe kwa kusisitiza mambo yafuatayo.

Kwetu sisi wanadamu, Mungu ni kama walivyo baba zetu hapa duniani. Kama ambavyo wazazi wetu waliotuzaa huturithisha mali, vile vile Mungu naye huwarithisha wanadamu baraka za aina mabalimbali.

Wapo watu maalumu wataostahili kurithi. Sio kwamba kila mtu anaweza kupewa urithi. La hasha. Wana ndio warithi halali wa mali za wazazi wao.

Mungu naye ana wana. Watu waliozaliwa mara ya pili, au waliookoka, hao ndio wana wa Mungu. Hao ndio wanaostahili kurithi baraka kutoka kwake.

Urithi kutoka kwa mwanadamu mmoja kwenda kwa mwanadamu mwingine una sheria, kanuni au taratibu zinazosimamia jambo hili. Hali kadhalika, urithi au baraka kutoka kwa Mungu una kanuni au masharti au taratibu zake.

Ili mtu aweze kurithi mali au baraka, ni lazima atimize masharti yanayotakiwa. Ni lazima atimize wajibu wake. Hakuna haki isiyokuwa na wajibu.

Mali yote wanayochuma wazazi huwaachia au huwarithisha wana wao. Kadhalika, kila alichoumba Mungu, ni kwa ajili ya mwanadamu, hasa wale wanaolicha jina lake. Yaani wale waliookoka.

Kama ambavyo mzazi huona fahari kumrithisha mwanawe mali, vile vile Mungu hufurahi sana wana wake wanapofanikiwa au wanapobarikiwa. Kiu ya Mungu ni kuona wanadamu wote wanaishi maisha ya fanaka. Ndio maana huwarithisha mali (Mithali 8:17-21).

Watu wengi, au tuseme wana wa Mungu, wanashindwa kurithi baraka kutoka kwake kwa sababu ya kutotimiza masharti yanayoambatana na baraka hizo.Wapo wengine wanaozitaka, lakini hawamtaki mwenye kuzimiliki. Hawataki kufanyika wana wa Mungu au kuokoka.

Kundi kubwa la waumini wanaoshindwa kurithi baraka kutoka kwa Mungu ni wale wasiofuata kanuni au wasiotekeleza masharti yanayoambatana na baraka wanazozitaka. Wengi hawamtolei Mungu kiasi cha kutosha au hawamtumikii kabisa, lakini bado wanataka kubarikiwa.

Msomaji ni matumaini yangu kuwa mada hii imekufungua macho kiasi cha kutosha. Kama ni urithi kutoka kwa wanadamu, naaamini sasa unatambua haki zako, na vile vile wajibu wako. Kwahiyo unajua la kufanya ili usipoteze haki hiyo.

Kama ni baraka kutoka kwa Mungu, napo naamini kwa sasa unatambua mambo unayoweza kupokea kutoka kwake, na vile vile wajibu wako au mambo unayotakiwa kuyafanya ili ubarikiwe kwa vitu vya rohoni na vya mwilini.

Rai yangu ni hii. Kama kuna eneo ambalo umegundua kuwa ulikuwa na mapungufu, tafadhali lifanyie kazi. Lirekebishe.

Kumbuka kuwa kama baba yetu wa duniani anavyompenda mwanawe, Mungu wetu naye ni mwema sana na siku zote anatuwazia yaliyo mema sisi tulio wana wake. Ukiona hayo mema aliyoahidi hayakufikii, ujue tatizo sio Yeye, bali ni wewe. Jirekebishe.

Lishike sana neno hili, :”Mungu si mtu, aseme uongo; wala si mwanadamu ajute; Iwapo amesema hatalitenda? Iwapo amenena, hatalifikiliza? (Hesabu 23:19). Wewe timiza wajibu wako, halafu usubiri wakati wa Bwana. Uwe mvumilivu, nawe utarithi baraka. Asante sana na Mungu wa mbinguni akubariki. Amen.

0 maoni:

Post a Comment

Tafadhali kuwa mstaarabu.
Jiheshimu kwa kutokuacha maneno yenye kauli ya kutusi ama kuudhi wengine.
Maoni yasiyofaa hayatachapishwa.

TaCHe & Subi.nukta77 chose to wear BlueWeed by BlogOh!Blog | to Blogger by Gre at Template-Godown | Entries (RSS) and Comments (RSS).