Friday, June 5, 2009

URITHI: Uchanga wa kiroho, wito na huduma katika baraka

Katika sehemu ya kwanza ya mada hii nilisema kuwa, mtoto mdogo hawezi kurithi mali kutoka kwa baba au mama yake, hata kama urithi huo ni haki yake. Nilianisha matatizo yanayoweza kujitokeza iwapo watoto watarithishwa mali.

Matatizo hayo ni pamoja na matumizi mabaya ya urithi uliopatikana, kama vile kutokujua nini cha kuufanyia, kutapanya, kudhulumiwa na kadhalika. Tunapogeukia urithi au baraka kutoka kwa Mungu tunakuta kuwa, hali inafanana sana na ile ya urithi kutoka kwa wanadamu.

Ukweli ni kuwa hata Mungu hawezi kuwarithisha watoto wadogo baraka, hata kama ni haki yao. Na watoto ninaozungumzia hapa ni waumini ambao tayari wameokoka, lakini bado ni wachanga kiroho au hawajakomaa katika mambo ya Mungu.
Mtoto mdogo haaminiki

Msomaji kama ukichunguza kwa makini utagundua kuwa, kuzaliwa kimwili kunafanana sana na kuzaliwa kiroho. Mtu anapozaliwa na wazazi wake, anaanzia utotoni na baadaye anakua (grow) mpaka anapofikia utu uzima. Baada ya kukua na kukomaa, ndipo anaweza kuaminiwa katika mambo makubwa, ikiwa ni pamoja na kukabidhiwa urithi wake.

Tunapozaliwa na Mungu au tunapookoka kwa mara ya kwanza, hiyo ni hatua ya mwanzo tu ya safari ndefu ya kuelekea mbinguni. Mkristo aliyeokoka, lakini hana siku nyingi katika wokovu, anakuwa hajui mambo mengi yanayohusu ufalme wa Mungu. Anakuwa hata tofauti na mtoto mdogo, ambaye bado hajaufahamu ulimwengu. Mkristo wa namna hiyo tunasema ni mchanga kiroho.

Mkristo ambaye bado ni mchanga, hawezi kuaminiwa katika maswala yanayohusu ufalme wa Mungu. Kwa mfano, hawezi kupewa nafasi ya uongozi (1Timotheo 3:6). Vile vile hawezi kurithishwa baraka mbalimbali zinazopatikana katika ufalme huu.

Biblia inasema nini kuhusu uchanga wa kiroho?

Hebu sasa tuigeukie Biblia tuone inasema nini kuhusu uchanga wa kiroho. Mtume Paulo anasema yafuatayo katika Wagalatia 4:19-20, “Vitoto vyangu, ambao kwamba nawaonea utungu tena mpaka Kristo aumbike ndani yenu; laiti ningekuwepo pamoja nanyi sasa, na kuigeuza sauti yangu! Maana naona shaka kwa ajili yenu”

Hawa watu ambao Paulo alisema nao maneno haya walikuwa ni watu wazima kimwili, lakini akawaita vitoto. Aliwapa jina hilo kwa sababu ingawa walikuwa wameokoka, bado walikuwa hawajakomaa katika maswala ya Mungu. Na kwa sababu hiyo alikuwa hawaamini.

Mstari wa 20 una maneno ‘maana naona shaka kwa ajili yenu’. Maneno haya yanaonesha kutoaminika. Kwahiyo Paulo alikuwa hawaamini wale waumini. Kisa? Bado walikuwa wachanga kiroho. Watu kama hawa huwezi kuwatweka majukumu mazito. Huwezi kuwarithisha baraka.

Watoto hawashirikishwi mambo mazito

Hebu tuangalie tena andiko lingine linalozungumzia uchanga wa kiroho na athari zake. Katika 1Wakorintho 3:1-2 mtume Paulo nasema kuwa, “Lakini, ndugu zangu, nami sikuweza kusema nanyi kama na watu wenye tabia ya rohoni, bali kama na watu wenye tabia ya mwilini, kama na watoto wachanga katika Kristo. Naliwanywesha maziwa sikuwalisha chakula; kwa kuwa mlikuwa hamjakiweza. Naam, hata sasa hamkiwezi”.

Msomaji unaweza kuona kuwa Paulo alishindwa kuongea na wale waumni mambo mazito ya kiroho kwa sababu walikuwa bado ni wachanga katika ufalme wa Mungu. Wasingemwelewa. Kwa sababu hiyo akaongea nao mambo mepesi mepesi tu. Yaani akawapa maziwa au uji au ‘mtori’, badala ya ugali.
Uchanga wa kiroho unatunyima uhondo

Ni ukweli ulio wazi kuwa, wakristo tunapoendelea kubaki watoto wachanga katika maswala yanayohusu ufalme wa Mungu, ndivyo tunavyoshindwa kufaidi uhondo ulio katika ufalme huu. Ndivyo tunavyoshindwa kurithi baraka mbalimbali.

Uchanga wa kiroho unatufanya tushindwe kufaidi mambo mazuri yaliyo ndani ya wokovu. Tunashindwa kula mema au manono ya nchi (Isaya 1:19). Tunashindwa kufanikiwa katika maisha ya kawaida hapa duniani.

Hili ndio moja ya matatizo makubwa yanayolikabili kanisa la Mungu sehemu nyingi duniani. Waumini hawakui na kukomaa katika mambo ya Mungu. Wanadumaa japo wameokoka. Na kwa sababu hiyo Mungu anashindwa kuwamwagia baraka kama alivyoahidi (Malaki 3:10).

Sikiliza ni kwambie kitu msomaji. Mungu wetu ana kiu kubwa sana ya kuturithisha baraka za rohoni na za mwilini. Kiu hiyo ni kubwa kuliko sisi wenyewe tunavyowaza au tunavyodhani (Waefeso 3:20). Tatizo letu ni kwamba bado hatujaweza kukaa mkao wa kubarikiwa. Bado tu watoto wadogo katika Kristo.
Mungu aweza kukunyima baraka kwa nia njema

Kama nilivyoainisha huko nyuma, zipo athari za kumrithisha mtoto mdogo baraka. Anaweza asimudu baraka atakazokabidhiwa. Kwa mfano anaweza kuzipoteza. Wengine zinawaleta kiburi na dharau. Na ukweli ni kuwa, Mungu akikuona huwezi kumudu au kukabiliana na baraka anazokusudia kukupa, hatakupatia.

Nia ya Mungu ya kukunyima hizo baraka ni ili usipotee. Ni ili usiwe mbali Naye. Wapo watu waliorithishwa baraka, lakini kwa sababu ya kiburi na dharau, wakashindwa kuendelea na wokovu. Wakamwasi Mungu halafu wakaipenda dunia. Matokeo yake wakafa katika dhambi.

Lengo kuu la Mungu katika maisha ya watu wake ni kuona kuwa wanarithi au wanaingia katika uzima wa milele. Baraka, aidha za rohoni au za mwilini, ni moja tu ya matunda ya wokovu. Lakini sio jambo ya msingi. Msingi ni kufika mbinguni.

Mungu yupo radhi kukuacha ukiwa maskini, iwapo anaona kwamba akikubariki, hutafika mbinguni. Na msomaji kama umewahi kuchunguza kwa makini, utagundua wapo watu waliobarikiwa, tena kidogo tu, lakini baada ya muda wakamwacha Mungu. Wakalewa mafanikio.


Kutotembea katika wito

Sababu ya nne na ya mwisho nitakayoizungumzia, ambayo inaweza kumnyima mwamini fursa ya kubarikiwa ni kutotembea katika wito alioitiwa na Mungu. Unakuta mtu huyo ameokoka, ni mwaminifu na hatendi dhambi yeyote. Hakosekani kanisani, lakini bado hali yake kimaisha au kiuchumi sio nzuri. Kwanini hali inakuwa hivyo?

Ukweli ni kuwa Mungu ametuokoa kwa makusudi maalumu. Kuna kitu au kazi au wajibu maalumu ambao kila mwamini amepangiwa na anatakiwa autimize kabla hajaondoka hapa duniani. Wajibu huo ndio unaitwa ‘wito wa Mungu’.

Hebu tuone Biblia inasema nini kwa habari ya wito. Katika 2Timotheo 1:9 tunaambiwa kuwa Mungu, “alituokoa akatuita kwa mwito mtakatifu, si kwa kadri ya matendo yetu sisi, bali kwa kadri ya makusudi yake yeye na neema yake”.

Huu mwito mtakatifu, ambao tunaambiwa ni kwa makusudi ya Mungu, ndio wito wenyewe.. Ni yale mambo ambayo anataka tuyafanye au tuyatimize katika maisha yetu ya wokovu hapa duniani. Huu ndio mwito mtakatifu au wajibu wetu maalumu kwa Mungu, na ni moja ya sababu iliyomfanya atuokoe.
Ndani ya wokovu kuna wajibu


Ukweli ni kuwa sisi hatukuokolewa ili kukae vivi hivi tu. La hasha. Hatukuokolewa ili tuburudike au tuifaidi matunda ya wokovu tu. Hapana. Yapo mambo ya kufanya; yapo majukumu; upo wajibu wa kutimiza.

Katika 1Petro 2:9 Biblia inasema hivi kuhusu watu waliookoka. “Bali ninyi ni mzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu, mpate kuzitangaza fadhili zake yeye aliyewaita mtoke gizani mkaingie katika nuru yake ua ajabu”.

Maneno ‘mpate kuzitangaza fadhili zake yeye aliyewaita mtoke gizani’ yanaonyesha kuwajibika. Yanaonyesha kwamba kila mtu aliyeokolewa na Mungu anapaswa kueneza habari hizi njema za wokovu kwa watu wengine ambao bado hawajaokoka.
Kanisa ni wapatanishi

Kila mtu aliyeokoka ni kuhani. Ni mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu ambao bado wapo dhambini. Anapaswa kuwahubiria au kuwashuhudia habari za Mwokozi Yesu (2Wakorintho 5:17-19) na za ufalme wa Mungu.

Mtume Paulo anasema yafuatayo kuhusu watu waliookoka kuwa wapatanishi. “Basi tu wajumbe kwa ajili ya Kristo, kana kwamba Mungu anasihi kwa vinywa vyetu; twawaomba ninyi kwa ajili ya Kristo mpatanishwe na Mungu” (2Wakorintho 5:20).

Pamoja na kila aliyeokoka kuwa mpatanishi, bado upo wajibu maalumu anaopaswa kuutimiza hapa duniani. Lipo eneo maalumu analotaka tumtumikie na sio kufanya chochote kile tunachoamua kwa matakwa yetu binafsi, hata kama kitu hicho ni kizuri.

Mwili mmoja, lakini viungo tofauti

Hebu tuangalie maana ya wito kwa kuangalia maumbile ya miili yetu. Katika Warumi 12:4-5 imeandikwa kuwa, “Kwa kuwa kama vile katika mwili mmoja tuna viungo vingi, wala viungo vyote havitendi kazi moja; vivyo hivyo na sisi tulio wengi tu mwili mmoja katika Kristo, na viungo, kila mmoja kwa mwenzake.”.

Sasa msomaji naomba uzingatie maneno ‘katika mwili mmoja tuna viungo vingi, wala viungo vyote havitendi kazi moja’. Kinachozungumziwa hapa ni kuwa, ingawa sisi sote tuliookoka ni wamoja katika mwili wa Kristo, lakini kila mmoja ni kiungo fulani katika mwili huo.

Nafikiri sote tunafahamu kuwa kila kiungo katika miili yetu kina kazi yake maalumu. Hakifanyi wala hakiwezi kufanya chochote kile kitakachopenda. La hasha. Kinaweza tu kufanya kazi moja kwa ufasaha.

Jicho haliwezi kusema; hiyo ni kazi ya mdomo. Mguu hauwezi kusikia, ingawa unaweza kutembea. Kazi ya kusikia ni ya sikio na ya kunusa ni ya pua, na kadhalika. Kila kiungo kina kazi yake maalumu na hakiwezi kufanya lolote lile linalohitajika kufanywa na mwili.

Hata swala la wito ndio lilivyo. Kwamba ingawa kila aliyeokoka ni kiungo katika mwili wa Kristo, lakini ipo kazi maalumu anayoweza na anayotakiwa aifanye. Akiifanya tunasema huyo anatumikia wito wake.
Wakristo wengi hawatambui wito wao

Kwa bahati mbaya wapo wakristo wengi sana ambao hawaelewi maana ya wito, wala hawajui wito wao ni upi. Kama nilivyosema, ni kweli wameokoka wala hawatendi dhambi (1Yohana 3:9). Lakini hawajui ni kazi ipi ambayo Mungu amewapangia na anatarajia waifanye.

Wapo waumini ambao wanafanya chochote kile ambacho nafsi zao zinawatuma kufanya. Hawamwulizi Mungu kama hicho wanachofanya ndicho anachotaka wakifanye au la. Yaani hawamwulizi wito wao ni upi? Hili ni tatizo kubwa kweli kweli katika kanisa la leo.

Sikiliza msomaji nikwambie kitu. Kila aliyeokoka anatakiwa atambue wito wake. Anatakiwa autafute uso wa Mungu mpaka amjulishe kile ambacho anamtaka akifanye. Halafu akiishatambua kitu hicho, au tuseme akishatambua wito wake, anatakiwa autumikie kwa bidii na kwa moyo mmoja. Hapo ndipo atakuwa ameyafanya mapenzi ya Mungu.

Kila mwamini ana kazi yake maalumu

Katika 1Wakorintho 12:28 tunaambiwa kuwa, “Na Mungu ameweka wengine katika Kanisa, wa kwanza mitume, wa pili manabii, wa tatu waalimu, kisha miujiza, kisha karama za kuponya wagonjwa, na masaidiano, na maongozi, na aina za lugha”.

Sio kila mtu aliyeokoka anaweza kuwa mtume, au nabii, au mchungaji, na kadhalika. Hapana. Wapo waumini maalumu walioteuliwa au waliochaguliwa na Mungu kwa ajili ya kufanya kazi kama hizi. Wanapotambua na kusimama katika nafasi zao, tunasema kuwa hawa wanatumikia wito wao.
Wito wa Paulo

Ili swala la wito liweze kueleweka vizuri, hebu tuchunguze utumishi wa Paulo. Nafikiri wengi wetu tunafahamu kuwa mtumishi huyu wa Bwana aliteuliwa na Mungu ili awe mtume. Jambo hili lipo wazi tunaposoma mistari ya mwanzo ya sura ya kwanza katika nyingi ya nyaraka zake.

Kwa mfano waraka kwa Wagalatia unaanza hivi. “Paulo, mtume, (si mtume wa wanadamu, wala kutumwa na mwanadamu, bali na Yesu Kristo, na Mungu Baba aliyemfufua kutoka wafu”. Hapa Paulo anatuonyesha kuwa yeye hakujichagua, wala hakuambiwa na wanadamu kwamba yeye ni mtume. Utume wake alipewa na Mungu kupitia kwa Yesu.

Paulo hakuwa mtume peke yake. La hasha. Vile vile alikuwa na karama au vipawa vya ualimu na uinjilisti. Jambo hili lipo wazi katika waraka au barua aliyomwandikia Timotheo, ambapo tunakutata na maneno ‘ambayo kwa ajili ya hiyo (yaani Injili) naliwekwa niwe mhubiri na mtume na mwalimu (2Timotheo 1:11).

Sasa msomaji nafikiri utakubaliana nami kuwa mwamini anaweza kuwa na karama au kipawa zaidi ya kimoja. Kama Paulo alipewa, hata leo hii sisi tuliookoka tunaweza kuwa na vipawa vingi. Ndio maana unasikia mtu anajiita mtume na nabii. Au mwingine ni mchungaji, mwinjililisti na vile vile ni mwalimu.
Usitumike popote pale

Tunapozidi kumchunguza Paulo tunaweza kuona kuwa yeye hakuwa mtume wa jumla jumla tu. Hapana. Yeye alikuwa ni mtume kwa ajili ya mataifa au watu ambao hawakuwa Wayahudi. Ndio maana alisafiri nchi nyingi akihubiri, akifungua makanisa na kufundisha.

Katika Warumi 11:13 Paulo aliandika maneno yafuatayo, “Lakini nasema na ninyi, mlio watu wa Mataifa. Basi, kwa kadri nilivyo mtume wa watu wa Mataifa, naitukuza huduma iliyo yangu”. Waweza pia kusoma Warumi 15:15-16 ambapo napo tunaona kuwa huduma au utume wa Paulo ulikuwa ni kwa ajili ya watu wasiokuwa Wayahudi.

Mtume Paulo alipojaribu kuwahubiria Wayahudi, walimkatalia au hawakumkubali (Matendo 13:46-48). Moja ya sababu iliyowafanya wasiikubali Injili yake ni kwa sababu alikuwa anatumika mahali ambapo hakupangiwa na Mungu. Alikuwa anahudumu nje ya wito wake, japo lilikuwa ni neno sahihi la Mungu.

Siku za leo kuna watumishi ambao huduma zao hazisongi mbele. Zimedumaa na hali za hao watumishi ni mbaya mno. Moja ya sababu inayoweza kuwafanya watumishi kama hao wawe na hali duni ni kwa sababu wanatumika nje ya wito wao.

Paulo alikuwa mwalimu wa somo la imani

Hebu tumrudie tena Paulo. Tumeona kuwa alikuwa na karama au kipawa cha ualimu. Lakini hakuwa mwalimu wa jumla jumla au wa kila somo. Hapana. Yeye alikuwa ni mwalimu wa imani. Ushahidi wa jambo hili ni waraka kwa Waebrania, ambao umesheheni maswala ya imani na inaaminika kuwa uliandikwa na mtume Paulo.

Vile vile Paulo mwenyewe anajishuhudia kama ifuatavyo katika Tito 1:1, “Paulo, mtumwa wa Mungu, na mtume wa Yesu Kristo; kwa ajili ya imani ya wateule wa Mungu, na ujuzi wa kweli ile iletayo utauwa. Kwahiyo Paulo alitambua nafasi yake. Alijitambua kuwa yeye ni mwalimu wa maswala ya imani.

Paulo hakuwa mwalimu wa imani tu. Hapana. Alifundisha masomo mengine pia. Alifundisha somo la ndoa, somo la karama, upendo, utoaji na kadhalika. Ninachotaka ujue msomaji wangu ni kuwa alijua kwa uhakika wito wake. Alijua kile ambacho Mungu alimtaka akifanye au afundishe.
Wapo watumishi ambao hawakuteuliwa na Mungu

Sasa hebu liangalie kanisa la leo. Unakuta wapo watu wanaojiingiza katika uchungaji, lakini hawakuteuliwa na Mungu kwa ajili ya kazi hii. Unakuta washirika au wanakijiji wanamshauri au wanamshinikiza mtu akawe mchungaji, naye anakubali bila hata ya kumwuliza Mungu ili apate kibali chake.

Wapo wachungaji wanaojiingiza katika huduma ya ualimu, kumbe hawana karama au kipawa hicho. Wengine wanajitia eti wanaweza kufundisha kila somo. Kwenye somo la imani wapo, kwenye somo la ndoa napo wapo, kwenye utoaji napo wapo na kadhalika.

Matokeo ya mtumishi kujitia gwiji wa kila kitu ni ubabaishaji makanisani. Waumini hawabarikiwi kwa sababu ya mafundisho dhaifu. Kanisa linakuwa na matatizo mengi na washarika hawakui kiroho.

Usijipachike kweye huduma

Huko nyuma nilisema kuwa karama na vipawa mbalimbali hutolewa na Mungu kwa njia ya Roho wake Mtakatifu. Nilisema kuwa wapo waumini ambao hutamani sana iwapo wangekuwa na karama au kipawa fulani. Wengine wanajipachika vyeo vya kitume, kinabii, kichungaji na kadhalika.

Biblia inaonyesha jinsi ambavyo watu wanaojipachika vyeo, karama au wanaotumikia wito usiokuwa wa kwao watakavyopata hasara siku ya hukumu ya Mungu. Yesu alisema “Si kila mtu aniambiaye, Bwana, Bwana, atakayeingia katika ufalme wa mbinguni; bali ni yeye afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni” (Mathayo 7:21).

Mapenzi ya Baba ni kile kitu ambacho Mungu anakutaka ukifanye. Ni wito wako. Sio unafanya chochote kile ambacho nafsi yako inatamani kukifanya. Ukienenda hivyo, unaweza kupata hasara ya milele.

Tahadhari usije ukakosa baraka ya uzima wa milele

Hawa watu ambao hawataingia katika ufalme wa mbiguni ni wale ambao walijiingiza katika kazi ambazo hawakupangiwa na Mungu. Wanaweza kuwa ni watumishi ‘feki’, au waumini waliotumika katika maeneo ambayo hayakuwa yao, japo walikuwa wameokoka.

Sikiliza Yesu anavyosema, “Wengi wataniambia siku ile, Bwana, Bwana, hatukufanya unabii kwa jina lako, na kwa jina lako kutoa pepo, na kwa jina lako kufanya miujiza mingi? Ndipo nitawaambia dhahiri, sikuwajua ninyi kamwe; ondokeni kwangu, ninyi mtendao maovu”. (Mathayo 7:22-23)

Sio kwamba watu kama hawa hawakumtumikia Mungu. La hasha. Walitumika, tena pengine vizuri tu. Ndio maana ishara na miujiza vilikuwa vinaonekana katika huduma zao. Lakini hawakuwasiliana na Mungu kuhusu aina ya utumishi aliowapangia. Hawakutumikia wito wao. Na kwa sababu hiyo watafukuzwa ili wasirithi uzima wa milele.

Ndani ya wito kuna baraka

Licha ya kutotambua wito ambao Mungu amewaitia, wapo waumini wengi sana wasiojua kuwa baraka zao zimeambatana au zimefungamanishwa na wito wao. Makanisani mwetu tunao waumini ambao ni waaminifu kwa Mungu na kwa viongozi wao, lakini bado hawaoni baraka zikiwajilia. Bado maisha yao ni duni. Moja ya sababu inayotufanya tusione mafanikio katika maisha ya wokovu ni kutotembea katika wito.

Ukweli ni kuwa, mwamini anapotembea katika wito au anapoyafanya mapenzi ya Mungu, ndipo anapoweza kuona baraka katika utimilifu wake. Ndipo anaweza kuwa karibu na Bwana, na kuuona uhalisi wake. Ndipo anapoweza kuufurahia wokovu wake. Vinginevyo ni mahangaiko matupu.

Ndani ya wito kuna mapito

Sina maana kuwa ukitumikia wito wako, hutakumbana na matatizo au majaribu. La hasha. Hayo yatakuwepo, maana ni sehemu ya kila aliyeokoka. Na ndio maana mtume Paulo anatuasa kuwa, “Maana mmepewa kwa ajili ya Kristo, si kumwamini tu, ila na kuteswa kwa ajili yake” (Wafilipi 1:19).

Unapotembea katika wito wako, Mungu atakuwa karibu sana na wewe. Ukipitia mambo magumu, msaada wake utapatika kirahisi zaidi kuliko mtu ambaye hatembei katika wito. Na mwisho wa yote utaona baraka tele katika maisha au utumishi wako.


Tafuta kuutambua wito wako

Nisikilize msomaji. Kama umeokoka, amani ya kweli haitakujia moyoni mwako mpaka pale utakaposimama katika wito wako. Wokovu nje ya wito ni mahangaiko mengi. Unaweza kupata mafanikio kiasi fulani, lakini hayatakuwa katika kile kiwango ambacho Mungu alikusudia. Huo ndio ukweli.

Ninayo changamoto kwako ndugu yangu unayesoma makala haya. Usikae kanisani mwako kijumla jumla tu baada ya kuokoka. Tafuta kuyajua mapenzi ya Mungu katika maisha yako ya wokovu. Tambua wewe ni kiungo gani katika mwili wa Kristo. Tambua kama wewe ni mkono, au mguu, au pua, au jicho, au sikio, na kadhalika. Huku ndio kutambua wito wako.

Baada ya kutambua wewe ni kiungo gani au wito wako, utumikie. Fanya kile ambacho Mungu anakutaka ukifanye, hata kama kiongozi wako au waumini wenzako watakuwa hawakuelewi. Kumbuka kuwa “Imetupasa kumtii Mungu kuliko wanadamu” (Matendo 5:29, 4:19).Ukimtii Mungu kwa kuyafanya mapenzi yake, ndipo utakapobarikiwa mno.

Barnaba na Paulo walimtiii Mungu

Ninazungumzia swala la kumtii Mungu kwa habari ya wito kwa sababu yawezekana mwamini akafanya maamuzi mabaya katika eneo hili. Kwa mfano anaweza kufuata ushauri wa kiongozi wake wa kidini au waumini wenzake, ambapo sio lazima ushauri huo uwe katika mapenzi ya Mungu.

Kumtii Mungu kunaweza kukufanya utengane na waumini wenzako. Kunaweza kukufanya uhame kanisa au kikundi au huduma uliyopo kwa sasa, halafu uhamie sehemu nyingine. Mfano mzuri ni Paulo na Barnaba, ambao iliwabidi watengane na waumini wenzao katika mji fulani, halafu wakaenda kuhudumu sehemu nyingine kama Mungu alivyowaagiza.

Tunasoma katika Matendo 13;2 kuwa, “Basi hawa walipokuwa wakimfanyia Bwana ibada na kufunga, Roho Mtakatifu akasema, Nitengeeni Barnaba na Sauli kwa kazi ile niliyowaitia”. Ujumbe huu ulitoka wakati Barnaba na Paulo wakiwa katika kanisa lililokuwa mji wa Antiokia. Ilibidi watengane na waumini wenzao, halafu waende kuhudumu katika miji ile ambayo walielekezwa na Bwana.

Wapo waumini waliopoteza mwelekeo

Leo hii wapo waumini walioacha kutumikia wito wao kwa sababu ya kuwasikiliza viongozi au ndugu na marafiki zao. Wapo wanaoona uzito wa kuhama sehemu fulani kwa sababu tu tayari wameshazoea sehemu hiyo na pengine tayari wana huduma fulani mahali hapo.

Linapokuja swala la wito, yawezekana mtu akaachana na wapendwa aliowazoea. au hali fulani ambayo inaonekana nzuri kwa wakati huo, ikabidi aende mahali pengine. Wakati mwingine hiyo sehemu nyingine inaonekana kama vile haina maslahi. Wito unahitaji kujikana nafsi na kuyafanya mapenzi ya Mungu kwa gharama yeyote ile (Marko 8:34).

Taji lako litategemea jinsi ulivyotumikia wito wako

Nafikiri kila mkristo mwenye matumaini ya kufika mbinguni anafahamu kuwa , baada ya kumaliza safari yake hapa duniani, atapewa taji ya uzima wa milele. Je, msomaji una habari kuwa uzuri wa taji yako itategemea jinsi ulivyotumikia wito wako hapa duniani?

Ukweli ni kuwa wakati wa kurithi uzima wa milele, sote hatutafanana. Wapo watakaong’ara kuliko wengine. Wapo watakaotukuzwa zaidi kuliko wenzao. Na kwa kiwango kikubwa, thawabu ya Mungu kwa wale watakaomaliza mwendo salama itategemea jinsi walivyotumika katika wito wao.

Je, haya ninayosema ni ya kweli? Je, yapo katika Biblia? Hebu tuangalie maandiko machache yanayoonesha jinsi tutakavyotofautiana wakati wa kurithi uzima wa milele. Kwahiyo msomaji naomba tufuatane kwa makini.
Tafuta dhahabu, usitafute manyasi

Tuanze na andiko la 1Wakorintho 3:11-15 linalosomeka hivi, “Maana msingi mwingine hakuna mtu awezaye kuuweka, isipokuwa ni ule uliokwisha kuwekwa, yaani, Yesu Kristo. Lakini kama mtu akijenga juu ya msingi huo, dhahabu au fedha au mawe ya thamanai, au miti au majani au manyasi, kazi ya kila mtu itakuwa dhahiri. Maana siku ile itaidhihirisha, kwa kuwa yafunuliwa katika moto; na ule moto wenyewe utaijaribu kazi ya kila mtu, ni ya namna gani. Kazi ya mtu aliyoijenga juu yake ikikaa, atapata thawabu. Kazi ya mtu ikiteketea, atapata hasara, ila yeye mwenyewe ataokolewa; lakini ni kama kwa moto”.

Hapa mtume Paulo anatujulisha kuwa msingi wa ufalme wa Mungu ni Yesu Kristo na kwamba kila mwamini anatakiwa ajenge juu yake. Anazidi kutuasa kuwa, tuwe makini na kile kitu tunachojenga juu ya huo msingi.

Unaweza kujenga hapo dhahabu, fedha, miti, manyasi na kadhalika. Yaani unaweza kujenga kitu cha maana au kitu cha hovyo. Nafikiri sote tunakubaliana kuwa aliyejenga hapo dhahabu atakuwa amefanya jambo jema kuliko yule aliyejenga fedha au majani. Dhahabu ina thamani zaidi.

Siku ya hukumu tutatofautiana

Ujenzi unaojengwa na mwamini unamaanisha jinsi anavyomtumikia Mungu katika maisha yake ya hapa duniani. Ni jinsi anavyoutumikia wito wake baada ya kuokoka. Anaweza kuutumikia vizuri au vibaya; au asiutumikie kabisa.

Maneno ‘Maana siku ile itaidhihirisha, kwa kuwa yafunuliwa katika moto; na ule moto wenyewe utaijaribu kazi ya kila mtu, ni ya namna gani’ yanazungumzia sikun yan hukumu. Yanaonesha kuwa siku ya hukumu kila mwamini atapimwa ni jinsi gani alivyomtumikia Mungu katika wito wake. Siku hiyo wengine watapata thawabu na wengine wataambulia hasara.

Katika 1Wakorintho 3:8 Paulo anazungumza maneno yafuatayo, “Basi yeye apandaye, na yeye atiaye maji ni wamoja, lakini kila mtu atapata thawabu yake mwenyewe sawasawa na taabu yake mwenyewe”

Hapa mtume Paulo anazungumzia utumishi wake na ule wa Apolo. Kwamba ingawa wote wawili walikuwa ni ndugu katika Bwana, lakini kila mmoja alikuwa na majukumu yake au wito wake. Vile vile kila mmoja wao atapata thawabu kulingana na jinsi alivyotumika ndani ya wito huo. Yaani watatofautiana wakati wa kuvishwa taji ya uzima wa milele.

Usikae bure, mtumikie Mungu

Mfano mwingine unaoonyesha jinsi watu wa Mungu tutakavyotofautiana wakati wa hukumu ya mwisho ni ule unaohusu kabaila aliyewapa watumwa wake fedha, ili wakazifanyie biashara. Huu unapatika katika injili ya Luka 19:11-26.

Kwa kifupi ni kuwa tajiri mmoja alisafiri, akawaachia watumwa wake fedha, ili wakazifanyie biashara na vile vile wapate faida. Kila mmoja wao alipewa kiasi kile kile cha fedha, yaani fungu moja.

Kitendo cha kupewa fedha ili wakazifanyie biashara ni sawa na kukabidhiwa majukumu. Ni kama vile Mungu anavyotupatia vipawa au karama, ili tukavitumie katika wito wetu. Sio tuvikalie kama yule mtumwa mwovu, ambaye alikalia fungu lake, badala ya kulifanyia kazi ((Luka 19:20-23).

Katika mfano huu tunaweza kuona kuwa yule tajiri aliporudi safarini, aliwazawadia wale watumwa kulingana na jinsi walivyozalisha faida. Yupo aliyepewa mamlaka juu ya miji kumi na mwingine juu ya miji mitano. Yule ambaye hakuzalisha, aliambulia patupu.

Hata katika ufalme wa Mungu ndivyo itakavyokuwa. Sote hatutalingana. La hasha. Wapo watakaong’aa kuliko wengine, kulingana na jinsi walivyomtumikia Mungu. Kulingana na jinsi walivyotumikia wito wao.
Kwanini Mungu huturithisha baraka?

Hivi msomaji umewahi kujiuliza ni kwanini Mungu huwarithisha wanadamu baraka, ziwe za rohoni au za mwilini? Ninapokaribia mwisho wa makala haya, naona ni bora nitaje sababu angalao mbili zinazomfanya Mungu aturithishe baraka sisi watu wake.

Sababu ya kwanza ni kwamba, vyote alivyoumba Mungu ni kwa ajili ya mwanadamu. Dunia na vyote viijazavyo ni mali ya Bwana (Zaburi 24:1). Lakini vitu hivyo vipo kwa ajili yako wewe na mimi msomaji wangu. Havipo kwa ajili ya Mungu.

0 maoni:

Post a Comment

Tafadhali kuwa mstaarabu.
Jiheshimu kwa kutokuacha maneno yenye kauli ya kutusi ama kuudhi wengine.
Maoni yasiyofaa hayatachapishwa.

TaCHe & Subi.nukta77 chose to wear BlueWeed by BlogOh!Blog | to Blogger by Gre at Template-Godown | Entries (RSS) and Comments (RSS).