Friday, June 5, 2009

Ni wakati gani wa kurithi baraka au ahadi za Mungu?

Katika sehemu ya kwanza ya mada hii nilisema kuwa, mara nyingi urithi kutoka kwa mwanadamu mmoja kwenda kwa mwanadamu mwingine unahusisha kifo. Kwamba ni lazima mmiliki wa kwanza wa mali inayokusudiwa kurithiwa afe, ndipo kitendo cha kurithi kifanyike.

Tunapogeukia urithi kutoka kwa Mungu kwenda kwa wanadamu tunakuta mambo ni tofauti kabisa. Sote tunafahamu kuwa Mungu hafi. Yeye alikuwepo tangu milele, na atadumu milele. Sasa kama hivyo ndivyo, swali la kujiuliza ni je, upi ndio wakati sahihi wa kurithi au kupokea ahadi kutoka kwa BWANA?

Mungu huwa hasemi siku kamili ya kukubariki

Ukweli ni kuwa, ukiichunguza Biblia kwa makini, utagundua kwamba Mungu huwa hasemi kwa yakini ni wakati gani atakapombariki au kumtimizia mtu ahadi aliyomwahidi. Hata kama mwamini ameiskikia sauti ya Mungu wazi wazi, ni mara chache sana ataambiwa muda kamili (exact time) wa kutimiziwa kile alichoahidiwa.

Tuseme umemtolea Mungu sadaka. Ni kweli Biblia inasema ukitoa utabarikiwa. Lakini huwezi kujua kama utabarikiwa baada ya mwezi mmoja, au mwaka mmoja, au miaka mitano au kumi. La hasha. Itakubidi usubiri hadi hapo majira au wakati wa BWANA utakapotimia, ndipo upokee mbaraka wako. Hii ndiyo hali halisi.

Jambo hili la kusuburi linahusu aina zote za baraka, yaani za rohoni na za mwilini. Tuchukulie mfano wa ujazo wa Roho Mtakatifu, ambao Biblia inaonyesha kuwa ni ahadi ya Mungu kwa watu waliookoka (Mdo 1:4, Mdo 2:14-18).

Baada ya kuokoka, mwamini hawezi kujua ni lini atajazwa Roho Mtakatifu. Wapo wanaojazwa siku hiyo hiyo waliyookoka. Wengine ni baada ya miezi au miaka kadhaa. Halafu wapo waliosubiri kwa muda mrefu mpaka wakakata tamaa kabisa. Wajibu wa mwamini ni kusubiri hadi hapo Mungu atakapoona vema kumjaza. Sio kukata tamaa.

Karama na vipawa hujitokeza baada ya muda mrefu

Linapokuja swala la karama, huwa hazijidhihirishi mara moja. Karama za neno la hekima, au maarifa, au uponyaji, au miujiza na kadhalika, huwa havionekani mara tu baada ya kuokoka. Mwamini anatakiwa adumu katika wokovu, ndipo baada ya muda vitu hivi vitaanza kujitokeza katika maisha yake.

Vipawa navyo huwa havijitokezi mara tu mtu anapookoka. Hapana. Mwamini hawezi kuokoka leo na kesho akaanza kusema yeye ni mtume au nabii au mchungaji na kadhalika. Ukiona hivyo ujue kuna walakini. Haya mambo huanza kujitokeza baada ya kudumu katika wokovu kwa muda wa kutosha.

Mitume, manabii, wachungaji, au wainjilisti tunaowaona leo hii wakinguruma katika madhabahu mbalimbali, hawakuanza huduma zao mara tu baada ya kuokoka. La hasha. Wengi walianza kama washirika wa kawaida tu makanisani mwao. Baadaye kabisa ndipo vipawa vyao vikaanza kuibuka.

Kwanini wakati wa kurithi baraka haujulikani?

Pengine msomaji unaanza kujiuliza ‘mbona wakati wa kurithi baraka kutoka kwa Mungu hauko wazi?’ Mbona Mungu huwa hasemi waziwazi wakati au siku atakayotubariki? Mbona mara nyingi baraka zenyewe zinakuja kama kwa kushitukiza? Nitajaribu kuleza baadhi ya sababu.

Ukweli ni kuwa mambo ya Mungu yana kanuni au taratibu zake. Hayajitokezi kienyeji au shaghalabaghala. La hasha. Yana mkondo wake. Na moja ya mkondo huo ni kanuni ya imani. Lakini kwa vipi haswa?

Ili tupate kuielewa kanuni ya imani, hebu tusome maana yake kama inavyojitokeza ndani ya Biblia. Katika Waebrania 11:1 tunaambiwa kuwa, “Basi imani ni kuwa na hakika ya mambo yatarajiwayo, ni bayana ya mambo yasiyoonekana”.

Haya mambo yanayotarajiwa, lakini bado hayajaonekana ni nini haswa? Ukweli ni kuwa, hizi ni baraka au ahadi mbalimbali, ambazo Mungu amewaahidi wanawe, yaani wakristo waliookoka. Ni ule urithi ambao Biblia inatamka wazi wazi kuwa Mungu atawapa wale wote watakaomwamini mwanawe Yesu Kristo. Haya ndiyo mambo ambayo yanatakiwa yakitokeze katika maisha ya mwamini.

Mungu hawezi kutoa ahadi ya uongo

Wajibu wa mwamini ili baraka za Mungu zijitokeze kwake ni kuamini kuwa ahadi zenyewe ni za kweli. Ni kuamini kuwa, “Mungu si mtu, aseme uongo; wala si mwanadamu, ajute; iwapo amesema hatalitenda? Iwapo amenena hatalifikiliza?’ (Hesabu 23:19).

Baada ya kuamini kuwa ahadi za Mungu ni za kweli, mwamini anatakiwa awe mvumilivu. Anatakiwa awe na subira, akitumaini kuwa kuna siku ahadi ya BWANA itatimia katika maisha yake, japo haijui siku hiyo. Huku ndiko kuiweka kanuni ya imani katika matendo.

Kwa kumalizia maelezo ya utendaji wa kanuni ya imani katika maisha ya mwamini naomba tusome Waebrania 6:17-18 ambapo tunaambiwa, “Katika neno hilo Mungu, akitaka kuwaonyesha zaidi sana warithio ile ahadi, jinsi mashauri yake yasivyoweza kubadilika, alitia kiapo katikati; ili kwa vitu viwili visivyoweza kubadilika, ambavyo katika hivyo Mungu hawezi kusema uongo, tupate faraja iliyo imara, sisi tuliokimbilia kuyashika matumaini yale yawekwayo mbele yetu.”

Kinachozungumzwa katika andiko hili ni kuwa Mungu akikuahidi kitu hawezi kubadilisha mawazo kirahisi. Hii ndiyo faraja yetu sisi tuliookoka. Kwamba tukiamini kile ambacho Mungu ametamka juu ya maisha yetu, basi tuishi kwa matumainin kwamba ipo siku kitu hicho kitajitokeza maishani mwetu, hata kama hatuijui siku hiyo.

Walio wachanga hawawezi kurithi

Pamoja na kutakiwa kuenenda kwa imani, vile vile yapo masharti au mambo mengine ambayo mwamini anatakiwa ayatimize, ndipo baadaye aweze kurithi baraka kutoka kwa Mungu. Tayari tumeshaona kuwa moja ya masharti hayo ni kukubali kuokoka. Sharti lingine ni kukua na kukomaa katika wokovu. Nitaeleza kwa kifupi.

Katika sehemu ya kwanza ya mada hii tuliona kuwa, mzazi hawezi kumpa mtoto mdogo urithi, hata kama ni stahili yake. Tulisoma andiko la Wagalatia 4:1 linalosema, “lakini nasema ya kuwa mrithi, wakati wowote awapo mtoto, hana tofauti na mtumwa, angawa ni bwana wa yote”.

Kinachozungumzwa hapa ni kuwa, mrithi hawezi kukabidhiwa mali yake wakati akiwa bado ni mtoto. Kwanza anatakiwa akue mpaka awe mtu mzima, ndipo aweze kukabidhiwa kilicho chake. Kwahiyo wakati akisubiri akue, anakuwa mtu asiye na kitu, japo ni tajiri.

Tunarithi baraka baada ya kukua kiroho

Nafikiri msomaji utakubaliana nami kuwa hakuna mzazi mwenye akili timamu atakayekubali kijana wake aoe, au atakayemwoza binti yake wakati bado ni mdogo. Nadhani wengi wetu tutakuwa tunafahamu jinsi serikali yetu inavyopiga vita tabia ya kuwaoza mabinti wenye umri mdogo. Wanatakiwa kwanza wakue na kukomaa miili na akili zao, ndipo waolewe.

Ni ajabu kwamba hata tunapogeukia urithi kutoka kwa Mungu, tunaweza kuona kuwa kuna kufanana na jinsi sisi wanadamu tunavyorithisha. Watoto wachanga kiroho hawawezi kurithishwa baraka kama vile karama au vipawa. Ni lazima kwanza wakue na kukomaa katika maswala ya ufalme wa Mungu, ndipo wanaweza kupokea baraka kama hizi.

Moja ya sababu inayomfanya Mungu asigawe baraka zake mapema ni kumpa mwamini nafasi ya kukua. Ni kumpa nafasi ya kulielewa vema neno la Mungu, kanuni na utendaji wake. Baada ya hapo ndipo anaweza kupewa baraka mbalimbali. Vinginevyo mwamini mchanga kiroho ni sawa na mtoto mdogo kimwili. Hawezi kurithishwa baraka kwa sababu zinaweza kumletea matatizo.

Tunarithi uzima wa milele baada ya kufa

Baraka kama ya uzima wa milele inarithiwa baada ya mwamini kufariki. Ni kweli kabisa baada ya kuokoka tunaamini kwamba tutafika mbinguni. Lakini jambo hili litakuwa kweli au dhahari baada ya kuondoka duniani kwa njia ya kifo. Kabla ya hapo, mtu aliyekiri wokovu anaweza kukwama njiani. Anaweza kushindwa kuvumilia hadi mwisho wa safari. Na kwa sababu hiyo asiweze kurithi uzima wa milele.

Mtume Paulo anaandika katika Wafilipi 3:12-14 kuwa, “Si kwamba nimekwisha kufika, au nimekwisha kuwa mkamililifu; la! Bali nakaza mwendo ili nipate kulishika lile ambalo kwa ajili yake nimeshikwa na Kristo Yesu. Ndugu, sijidhanii nafsi yangu kwamba nimekwisha kushika; ila natenda neno moja tu; nikiyasahau yalio nyuma, nikiyachuchumilia yaliyo mbele; nakaza mwendo, niifikilie mede ya thawabu ya mwito mkuu wa Mungu katika Kristo Yesu”.

Tukaze mwendo
Paulo alipoandika maneno haya alikuwa tayari ameokoka. Lakini vile vile alitambua kuwa bado hajaingia katika uzima wa milele. Alitambua kwamba bado yupo safarini na kwamba anapaswa kujitahidi. Vinginevyo anaweza asimalize mwendo. Anaweza asifike hatua ya kurithi uzima wa milele.

Yesu alisema katika Mathayo 24:13 kuwa,”Lakini mwenye kuvumilia hata mwisho, ndiye atakayeokoka”. Mwisho unaozungumziwa hapa unaweza kuwa ni mwisho wa maisha ya mwamini hapa duniani, yaani kifo. Au ni wakati wa kunyakuliwa kwa kanisa wakati Yesu atakaporudi duniani mara ya pili.

Mwamini atakapofikia mwisho wake salama, ndipo atakuwa na uhakika wa kurithi uzima wa milele. Kwahiyo tunatakiwa tukaze mwendo kama Paulo. Vingine safari ya mbinguni inaweza kuwa ni ndoto za alinacha. Tunaweza tusifike huko, japo tuanasema tumeokoka.

0 maoni:

Post a Comment

Tafadhali kuwa mstaarabu.
Jiheshimu kwa kutokuacha maneno yenye kauli ya kutusi ama kuudhi wengine.
Maoni yasiyofaa hayatachapishwa.

TaCHe & Subi.nukta77 chose to wear BlueWeed by BlogOh!Blog | to Blogger by Gre at Template-Godown | Entries (RSS) and Comments (RSS).