Monday, May 11, 2009

MKRISTO NA MAVAZI: Utangulizi

DHAMBI YA BATH-SHEBA: JE, MUNGU ANAJALI JINSI NINAVYOVAA?

Utangulizi
Mtu yeyote akichunguza Biblia kwa makini atagundua kuwa Mungu wetu ni wa utaratibu. Atagundua kuwa Mungu hafanyi mambo au mapenzi yake kienyeji tu. Hapana. Hafanyi jambo kwa kubahatisha. La hasha. Atagundua kuwa Mungu huwa anafuata utaratibu fulani aliojiwekea yeye mwenyewe.

Kwa mfano, tunapoangalia jinsi alivyoumba dunia na vyote viijazavyo, tunaona kuwa alifanya hivyo hatua kwa hatua. Alifuata utaratibu wa ni jambo lipi lifanyike siku ya kwanza na ni lipi lifanyike siku ya sita au siku ya mwisho. Hakuwa tu anaumba ali mradi vitu viwepo. Hapana hata kidogo.

Unapozidi kuichunguza Biblia utagundua kuwa Mungu amempa mwanadamu uhuru wa kumtosha kwa ajili ya kuendesha maisha yake hapa duniani. Lakini pamoja na kumpa uhuru wa kutosha, vile vile amemwekea mipaka fulani fulani ambayo hapaswi kuivuka. Kuna mambo ambayo amemkataza asiyafanye.

Mungu hakutuacha tujiendee tu kama tunavyotaka. La hasha. Hakutuacha tuogelee tu bila kizuizi chochote. Hii imekuwa ni tabia ya Mungu tangu alipoumba dunia na viumbe vyote viijazavo, ikiwa ni pamoja na wanadamu. Hakumpa mwanadamu uhuru wa kujifanyia mambo yake au kujiendea vyovyote vile anavyotaka bila mipaka yoyote.

Sio tu kwamba Mungu amemwekea mwanadamu mipaka, bali vile vile amemwagiza mambo fulani fulani. Yapo mambo ambayo Mungu ametuagiza sisi wanadamu tuyafanye na mengine ametukataza tusiyafanye. Yale mambo aliyotuagiza tufanye ni kwa ajili ya makusudi yake na wakati wote yanakuwa na faida kwetu sisi tunaoyafanya.

Mara nyingi yale aliyotukataza ni kwa ajili ya manufaa yetu. Mungu anajua kuwa yapo mambo ambayo tukiyafanya tutadhurika au tutapata hasara. Tutajikuta mahali pabaya. Kwahiyo anapotukataza anakuwa na lengo zuri la kutuepusha na matatizo, japo kwa akili zetu za kibinaadamu tunaweza tusitambue hayo makusudi mazuri ya Muumba wetu. Na wakati mwingine huwa haelezi bayana ni kwanini anatukataza jambo fulani.

Tunapoangalia kitabu cha Mwanzo 2:16 tunaona kuwa Mungu alipomwumba Adamu na kisha kumweka katika bustani ya Eden, alimpa uhuru wa kula matunda yote yaliyokuwa ndani ya ile bustani, isipokuwa matunda yaliyotokana na mti wa ufahamu wa mambo mazuri na mambo mabaya. Biblia inatuambia kuwa, “Bwana Mungu akamtwaa huyo mtu, akisema, matunda ya kila mti wa bustani waweza kula, walakini matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula matunda ya mti huo utakufa hakika”.

Katazo la kutokula matunda yaliyokuwa katika mti wa ujuzi wa mambo mema na mabaya ni mojawapo wa aina ya mipaka ninayozungumzia. Kwamba Adamu alikuwa na uhuru wa kumtosha kabisa wa kula matunda ya miti mingine yote iliyokuwa bustanini, isipokuwa matunda ya huo mti mmoja tu. Mungu alijua kwamba kutakuwa na madhara iwapo Adamu atakula matunda ya mti wa ujuzi wa mambo mema na mabaya. Ndio maana alimkataza asiyale.

Kwa bahati mbaya Adamu alishindwa kutii agizo la Muumba wake. Yeye alivuka mpaka aliokuwa amewekewa kwa kile kitendo chake cha kula matunda aliyokuwa amekatazwa. Hakujua ni madhara gani yatakayotokea iwapo atakula hayo matunda. Na kama sote tunavyojua ni kwamba, matokeo ya Adamu kushindwa kutii agizo la Mungu ni dhambi kuingia ulimwenguni.

Sina haja ya kuelezea madhara ya dhambi humu duniani, kwani naamini wengi wetu tunayafahamu. Lakini kwa kifupi tu ni kuwa madhara hayo ni laana kwa wanadamu, ardhi na viumbe alivyoumba Mwenyezi Mungu (Mwanzo 3:14-19). Ndio hizi taabu na mahangaiko tuliyo nayo ulimwenguni kwa sasa. Ni pamoja na mauti inayowapata wanadamu, jambo ambalo halikuwa limekusudiwa na Mungu wakati wa uumbaji wake. Hakika uasi wa Adamu uliiletea dunia hasara kubwa.

Hata sasa uasi wa mwanadamu unaendelea kuifanya dunia isiwe mahali salama pa kuishi. Wanadamu bado hawajaacha tabia ya kuyaasi maneno au maelekezo ya Mungu. Uasi umeendelea kudumu tangu mwanzo wa ulimwengu huu hadi sasa. Kwa bahati mbaya anayepata hasara kadri uasi unavyoendelea kudumu ni mwanadamu na wala sio Mungu.

Kama nilivyosema ni kuwa Mungu ni wa utaratibu. Kila agizo lake lina sababu zake. Sisi kama wanadamu tunaweza tusielewe ni kwanini anatuagiza jambo fulani. Lakini ukweli ni kuwa kila nyuma ya agizo litokalo kwa Mungu, ipo sababu ya msingi kabisa iliyomfanya atoe agizo hilo. Usipotii agizo lake, utajikuta matatani. Wewe ndiye utakayepata hasara.

0 maoni:

Post a Comment

Tafadhali kuwa mstaarabu.
Jiheshimu kwa kutokuacha maneno yenye kauli ya kutusi ama kuudhi wengine.
Maoni yasiyofaa hayatachapishwa.

TaCHe & Subi.nukta77 chose to wear BlueWeed by BlogOh!Blog | to Blogger by Gre at Template-Godown | Entries (RSS) and Comments (RSS).