Monday, May 11, 2009

MKRISTO NA MAVAZI: Eti Mungu anaangalia moyo tu?

JAMANI ETI MUNGU ANAANGALIA MOYO TU?

Hebu tuanze na sehemu ya barua ya msomaji anayeitwa Isope Mwakibasa iliyokuwa na kichwa cha habari kama ilivyo hapo juu, na ambayo iliyotokea katika Gazeti la Kikristo la Nyakati. Nanukuu kama ifuatavyo;

………………… Kuna mambo mengi sana ambayo yamekuwa yakihaririwa (kusahihishwa) sana kwenye Biblia na kuonekana kwamba wale walioandika ni watu wa zamani sana (wamepitwa na wakati) ambao mambo mengi waliyoyaandika yalifaa kwa kipindi kilichopita na sasa ni wakati wa Sayansi na Teknolojia. Walokole wengi wamekuwa wakisahihisha maneno ya MUNGU ili waweze kutimiza matakwa yao na wala si ya MUNGU.
Leo nitalitolea mfano jambo moja tu ambalo limekuwa ni tatizo kubwa sana kwa kanisa la leo. Jambo hili linatetewa sana na wakristo pamoja na makanisa na viongozi wa juu wa dini hii kwa kuwafundisha waumini wao ambao wako tayari kwenda Jehanamu na makundi yao kuliko kulikosa kwa kisingizio kuwa watachekwa na mataifa mengine, eti kwa kutokwenda na wakati.
Jambo lenyewe ni kuhusu mavazi ya kiume na ya kike. Mabinti, wamama na vijana wa kiume wa Kikristo (walokole) wa sasa ambao wanadai kuwa wako safarini kwenda mbinguni, leo hii kuvaa mavazi yasiyo ya jinsia yao ni jambo la kawaida. Ukisoma katika Kumbukumbu la Torati 22:5 neno la MUNGU linasema “Mwanamke asivae mavazi yampasayo mwanaume, wala mwanaume asivae mavazi yampasayo mwanamke; kwa maana kila afanyaye mambo hayo ni machukizo kwa BWANA, MUNGU wako”.
Sasa mimi nimekuwa nikijiuliza sana bila kupata majibu kuhusu hawa wamama. Je, andiko hili hawalioni? Na je, kama wanaliona, inakuwaje vijana wa kiume na mabinti wanavaa mavazi haya? Nimewahi kuwauliza baadhi ya mabinti na wamama kadhaa, ikiwa ni pamoja na baadhi ya wajiitao kuwa ni watumishi wa MUNGU kuhusu uvaaji wa mavazi yasiyo yao, kama wamewahi kuliona andiko hilo ama la! Wengi wamekuwa wakiliona na kulisoma sana, ila ni ujeuri na kiburi cha uzima ndani ya mioyo yao. Majibu niliyokutana nayo hayamo kwenye Biblia bali ni historia na unafiki wa mtu ikiwa ni pamoja na ulimwengu unavyokwenda. Kati ya hao ambao nimekuwa nikizungumza nao kuhusu suala hilo wamekuwa wakijitetea kwa kusema kuwa, suruali si vazi la kiume bali ni la watu wote, Vilevile suruali ni vazi la heshima sana kwa mtu wa jinsia yoyote kuliko vazi lingine lolote kwa maana hata nikianguka sikai wazi.
Mwingine alijitetea kwa kueleza kuwa Taifa la Israeli, ambalo ni taifa la MUNGU, alisema kuwa askari wa Kiyahudi wa kiume wanavaa sketi na wale wa kike wanavaa kaptula. Sasa iweje kwa mataifa mengine iwe ni vibaya. Akasema huko si kumkosea MUNGU maana ameruhusu kwa taifa lake wavae kama mataifa mengine wavaavyo.
Wengine ukiwauliza kuhusu jambo hilo wanakuwa wakali na kusema kuwa mambo mengine yaliyoandikwa enzi zile si yote ya kutumika kwa nyakati hizi za sasa, bali yalikuwa ya wakati ule. Kwa sasa ni lazima wakristo tubadilike na kuenenda kama ulimwengu unavyokwenda na wala si kung’ang’ania mambo ya kishamba.
Jamani tangu lini mambo ya MUNGU yakaenda na wakati? Akina kaka nao hawako nyuma. Kukutana ama kuwaona vijana wa kiume wakiwa wamevaa hereni ama kusuka nywele nalo ni jambo la kawaida siku hizi. Wengine husema kuwa MUNGU anaangalia moyo haangalii mavazi ya mtu wala kitu kingine chochote. Jamani jamani! Kweli Mungu anaangalia moyo tu na wala si mwenendo au matendo ya mtu na mavazi kweli? MUNGU atusaidie sana katika hili. ……….(Mwisho wa kunukuu).

Mambo muhimu yanayojitokeza katika barua hii
Hebu tuangalie mambo muhimu yanayojitokeza katika barua hii. Nitajaribu kuyaandika kwa kifupi kama ifuatavyo;
  • Wapo wakristo waliookoka, lakini wanalihalifu neno la Mungu linaloweka mipaka kati ya mavazi ya kike na ya kiume.
  • Wapo wakristo waliotekwa na tamaa au nia ya kutaka kwenda na wakati katika mambo mengi, ikiwa ni pamoja na eneo la mavazi.
  • Wapo viongozi na waumini wanaotetea kwa nguvu zao zote uvaaji ulio kinyume na maagizo ya Mungu.
  • Kuna sababu za aina mbalimbali zinazowafanya wakristo wavae mavazi yaliyo kinyume na maagizo ya Mungu.

0 maoni:

Post a Comment

Tafadhali kuwa mstaarabu.
Jiheshimu kwa kutokuacha maneno yenye kauli ya kutusi ama kuudhi wengine.
Maoni yasiyofaa hayatachapishwa.

TaCHe & Subi.nukta77 chose to wear BlueWeed by BlogOh!Blog | to Blogger by Gre at Template-Godown | Entries (RSS) and Comments (RSS).