Tuesday, May 12, 2009

MKRISTO NA MAVAZI: Dhambi ya Bath-sheba

Katika kuelimishana juu ya jambo hili la mavazi, nitatoa maelezo marefu kidogo. Lakini kimsingi nitatumia kisa kimoja maarufu sana kilicho ndani ya Biblia. Hiki kinamhusu mfalme Daudi na mwanamke mmoja aliyeitwa Bath-sheba. Na kwa mantiki ya lengo la makala haya, nimekipa kisa hicho kichwa cha habari kinachosema ‘Dhambi ya Bath-sheba’.

Kisa chote kinachohusu mkasa wa Daudi na mwanamama Bath-sheba kinapatikana katika 2Samweli sura ya 11 na ile ya 12. Hebu tujikumbushe maneno machache ya kisa hiki. Biblia inatuambia kuwa, “Ikawa wakati wa jioni, Daudi akaondoka kitandani, akatembea juu ya dari ya jumba la mfalme; na alipokuwa juu ya dari aliona mwanamke anaoga; naye huyo mwanamke alikuwa mzuri sana, wa kupendeza macho. Naye Daudi akapeleleza, akauliza habari za yule mwanamke. Mtu mmoja akasema, Je! Huyu siye Bath-sheba, binti Eliamu, mkewe Uria, Mhiti? Basi Daudi akapeleka wajumbe, akamtwaa; naye akaingia kwake; naye akalala naye; kisha akarudi nyumbani kwake” (2Samweli 11:2-4).

Hapa tunamwona mfalme wa Israeli akivutwa na uzuri wa sura na umbile la mwanamke aliyekuwa akioga. Mwanamke yule alikuwa uchi. Baada ya kumwona tu, Daudi aliwaka tamaa kiasi ambacho alishindwa kabisa kujizuia. Matokeo yake alimchukua yule mwanamama aliyeitwa Bath-sheba, ambaye pia alikuwa ni mke wa mwanajeshi mmoja aliyeitwa Uria, kisha akazini naye.

Watu wengi wanapoelezea kisa hiki huwa wanapenda sana kuonesha kosa au dhambi ya Daudi ya kuzini na mke wa mtu. Huwa hawaoni kabisa kosa la Bath-sheba. Yeye anaonekana kuwa hakuwa na hatia yoyote. Hata mimi kwa kiwango fulani sipingani na wazo kama hilo, kwamba kweli mfalme Daudi alitenda dhambi. Lakini hebu leo tutazame kwa sura nyingine kabisa mazingira ya kisa hiki, ambacho kilimsababisha mfalme na heshima zake zote, aanguke katika dhambi ya uzinzi.

Ni kweli kabisa kuwa mfalme Daudi alitenda dhambi, tena ya kukusudia. Hakujali utu wa mtu mwingine. Hakuonyesha ubinadamu, hata baada ya kuambiwa kuwa yule alikuwa ni mke wa mtu. Ni kweli kabisa alifanya ukatili wa hali ya juu wa kulala na huyo mwanamke na kisha baadaye akamwua mumewe. Hilo silikatai; maana hata Mungu mwenyewe aliuelezea ukatili huo kwa kutumia kinywa cha nabii Nathani. Vile vile alimpatiliza Daudi kwa kosa hilo (2Samweli 12:1-23).

Lakini papo hapo kuna kosa alilolifanya Bath-sheba, hata kama hakufanya kosa hilo kwa kukusudia, kama ilivyokuwa kwa mfalme Daudi. Ukweli ni kuwa, bila kukusudia wala kuwa na nia yoyote mbaya, Bath-sheba alijiacha uchi mbele ya mwanamume aliyeitwa Daudi. Huyu mwanamume alipomwona, alishindwa kabisa kujizuia. Matokeo yake akajikuta tayari ameshamtenda Mungu wake dhambi (2Samweli 12:13).

Ni vigumu sana kuliona kosa la Bath-sheba. Kama nilivyosema ni kwamba, mwanamke huyu, kwa mtizamo wa nje, hakuwa na nia yeyote mbaya. Hakuwa na mpango wa kujionyesha mbele ya Daudi, wala kumvuta kwa uzuri wa maumbile yake. Lakini bado kitendo chake cha kukaa uchi kilimwangusha mwanamume wa watu katika dhambi ya uzinzi, hata kama kosa hilo lilitendeka pasipo kukusudia (unintentional).

Laiti mwanamama yule angekuwa makini kidogo tu; laiti angechunguza mazingira yaliyokuwa yanamzunguka kabla hajavua nguo zake. Laiti angeinua macho yake na kuangalia juu, pengine angemwona mfalme Daudi na kwa sababu hiyo asingevua nguo. Kwa bahati mbaya hilo halikutokea kwa siku ile. Na hilo ndio kosa au dhambi ya Bath-sheba. Kutokuwa mwangalifu. Ndipo madhara yakatokea. Tena madhara makubwa mno.

 
Dhambi ya Bath-sheba ilileta madhara makubwa sana
Dhambi au kosa la Bath-sheba ni dogo sana ukilinganisha na lile la Daudi. Lakini pamoja na hayo, dhambi ile ilileta madhara makubwa sana. Ukiendelea kuchunguza kisa chote kwa makini utagundua kuwa licha ya kusababisha uzinzi, pia yapo madhara mengine yaliyojitokeza. Kulitokea mauaji ya mtu asiyekuwa na hatia (Uria). Jina la Bwana lilitukanwa kutokana na mpakwa mafuta wa Bwana (Daudi) kuanguka katika dhambi.

Baada ya uzinzi ule, mtoto haramu alizaliwa na vile vile akafa. Uasi ulitokea nyumbani mwa Daudi na kusababisha aibu kubwa ya Absalomu (mwana wa mfalme) kulala na wake za babaye, tena mbele ya kadamnasi ya Waisraeli. Kulitokea laana ya upanga kutoondoka katika nyumba ya Daudi, ubakaji, mauaji na kadhalika. Yaani amani ilitoweka kabisa nyumbani mwa mfalme Daudi.

Upo msemo wa Kiingereza unaosema, “Behold how great a matter, a little fire kindleth”. Yaani ‘tazama ni jinsi gani moto unaoonekana kuwa mdogo tu na usio na dhara lolote, unavyoweza kusababisha jambo kubwa bila kutarajiwa’. Waswahili wanasema ‘mdharau mwiba humchoma’.

Biblia kwa kuungana na huo msemo wa Kiingereza una haya ya kutuonya, “Angalieni, twatia lijamu katika farasi, ili wamtii, hivi twageuza mwili wao wote. Tena angalieni merikebu; ingawa ni kubwa kama nini, na kuchukuliwa na pepo kali, zageuzwa na usukani mdogo sana, kokote anakoazimia kwenda nahodha. Vivyo hivyo ulimi nao ni kiungo kidogo, nao hujivuna majivuno makuu. Angalieni jinsi moto mdogo uwashavyo msitu mkubwa” (Yakobo 3:3-5).

Lijamu (kipande cha chuma kinachopitishwa katikati ya midomo ya farasi ili kufungia hatamu au kamba za kumwongozea) ni kitu kidogo sana ukilinganisha na ukubwa wa farasi mwenyewe. Lakini ni kupita hiyo lijamu, ambapo mwili mzima wa farasi hugeuzwa. Usukani wa merikebu ni mdogo sana ukilinganisha na ukubwa wa merikebu yenyewe. Lakini ni usukani huo huo unaogeuza chombo kizima pamoja na ukubwa wake wote.

Yanayoelezwa hapa ndiyo yaliyotokea kumhusu Bath-sheba. Kosa dogo tu (tena lisilo la kukusudia) la kukaa uchi mbele ya mwanamume, lilisababisha madhara makubwa mno. Jambo lililoonekana kuwa ni la kawaida tu, bado jambo hilo likaleta madhara makubwa mno. Hata leo hii swala la mavazi yasiyofaa linaweza kuonekana ni jambo dogo tu. Lakini je, ni madhara kiasi gani yanayoletwa na wanawake wanaotembea nusu uchi barabarani?

Matatizo yaliyompata Daudi, familia yake na taifa la Israeli yasingetokea iwapo Bath-sheba angekuwa makini kidogo. Laiti angekuwa makini na mahali au muda wa kuoga, pengine Daudi asingemwona akiwa uchi. Laiti asingeogea nje mahali pa wazi au kama angeenda kuoga usiku badala ya mchana, ni saa ngapi Daudi angemwona katika hali ile hata amtamani? Lakini maskini, tahadhari haikuwepo. Bila kutegemea, kosa dogo tu la kutokuwa makini, likasababisha adha kubwa.


Makanisani tunao akina Bathisheba wengi
Kinachonisukuma kuandika makala haya ni kuwa, ndani ya makanisa yetu, tunao akina Bathi-sheba. Tena siku hizi ni wengi mno. Katikati ya jamii ya wakristo, wapo wanawake wanaokiri wokovu, lakini kwa kutokujua au kwa uzembe, wanajiacha nusu uchi. Wanavaa mavazi yanayoianika miili yao nje nje; na kwa sababu hiyo wanakuwa kwazo kwa washirika wenzao, hasa wanaume.

Sisemi kuwa hawa wanawake wote wanaovaa mavazi yasiyofaa wanafanya hivyo kwa makusudi. La hasha. Ninajua kuwa wengine wao ni wacha Mungu wazuri mno. Wengine ni wa kiroho vizuri kabisa na sio wazinifu hata kidogo, wala hawawi na nia yoyote mbaya wakati wanapovaa hizo nguo za aibu. Tatizo lao ni ile kutotambua madhara yanayoletwa na huo uvaaji wao.

Ukweli ni kwamba, makanisani mwetu tunao wanawake wapendwa ambao hawako makini na aina ya mavazi wanayovaa. Wapo wanaovaa nusu uchi; na kwa sababu hiyo tayari wamekuwa kwazo kwa wanaume wengi. Tayari wamekuwa ni sababisho la madhara kama yale yaliyoletwa na Bath-sheba kwa mfalme Daudi.

Ninachomaanisha ni kuwa wapo wanaume walioanguka katika uzinzi kwa sababu ya tamaa zao kuamshwa na hao wanawake wasiovaa mavazi ya heshima. Unaweza kuwa ni uzinzi wa macho au ule wa kufanya tendo lenyewe kabisa. Vyovyote vile iwavyo, uzinzi unakuwa umetokea. Hili nitaeleza kwa kirefu zaidi huko mbeleni.

Leo hii ukichunguza makanisa mengi utagundua kuwa uvaaji wa baadhi ya wanawake umevuka mipaka. Wanawake hawa wanavamia kila ‘fasheni’ au mitindo ya mavazi bila kujali kuwa baadhi ya mitindo hiyo ipo kinyume na maagizo ya Mungu. Kwa sababu hiyo basi, ipo haja ya kupambana na tatizo hili kabla halijakomaa na kulimeza kanisa la Bwana.

2 maoni:

Rule Budodo said...

Enter your comment...umenibaliki sana,hata mm nlikuw slion kosa la bath-sheba.mungu ak ubarki sana na endlea kuelmsha wakristo

Rule Budodo said...

Be bleced so much, even me i didn't saw bathsheba's sin but thank u, u hav made me to undertand that.

Post a Comment

Tafadhali kuwa mstaarabu.
Jiheshimu kwa kutokuacha maneno yenye kauli ya kutusi ama kuudhi wengine.
Maoni yasiyofaa hayatachapishwa.

TaCHe & Subi.nukta77 chose to wear BlueWeed by BlogOh!Blog | to Blogger by Gre at Template-Godown | Entries (RSS) and Comments (RSS).